Wednesday, July 30, 2014


Athuman Idd 'Chuji' baada ya kuikosa Azam fc sasa anasaka nafasi ya kusajiliwa JKT Ruvu

Na Baraka Mpenja, Dar es salaam

Imechapishwa Julai 30, 2014, saa 10:48 jioni

WANANDINGA waliotamba na klabu za Yanga, Simba na Azam fc wanafanya majaribio chini ya kocha mkuu wa JKT Ruvu, Fredy Felix Minziro kwa lengo la kutafuta nafasi ya kusajiliwa kwa ajili ya msimu wa 2014/2015 wa ligi kuu soka Tanzania bara.
Meneja wa JKT Ruvu, Joel Frank Cibaya ameiambia MPENJA BLOG jioni hii kuwa wachezaji wanaofanya mazoezi kwa muda mrefu sasa ni Henry Joseph Shindika, Haruna Ramadhani Shamte, Betram Mombeki na Jackson Chove.
Pia Cibaya alimtaja aliyekuwa kiungo mahiri wa Yanga, Athuman Idd `Chuji` kuwa anajitokeza mara kadhaa katika mazoezi hayo.
Betram Mombeki kutoka Simba sc anaendelea kujaribu bahati yake JKT Ruvu.

“Wapo wachezaji wanaofanya mazoezi hapa. Na kwa bahati nzuri TFF wamesogeza ligi mbele imekuwa ni nafasi nzuri ya kuwaangalia,”Alisema Cibaya.
“Mwalimu kuna wachezaji anawatazamia. Kama unavyojua ana uzoefu na wachezaji wa timu kubwa. Hakuna watu wasumbufu kama wachezaji wa timu kubwa hususani kutoka Simba na Yanga”
“ Kwasababu wale hawaamini kama wapo JKT Ruvu au wako Mtibwa. Wanadhani maisha ya Simba na Yanga ndio yapo JKT Ruvu, kwahiyo wanapovikosa vitu walivyopata Simba wanakuwa wasumbufu zaidi”.
Katika hatua nyingine, Cibaya aliwataja wachezaji waliosajiliwa kwa maana ya raia na askari kuelekea msimu mpya wa ligi kuu unaotarajia kuanza kutimua vumbi septemba 30 mwaka huu.
Jabir Aziz (kushoto) anafanya majaribio JKT Ruvu

Wachezaji raia waliosajiliwa na JKT Ruvu ni: Ambrose Morris (kutoka Zanzibar), Mohamed Faki (Ashanti) na Benjamin Haule (Ruvu Shooting).
Wachezaji askari (wanajeshi) waliosajiliwa ni: Madenge Ramadhani, Issa Kanduru, Nafo Sanane na Nurdin Mohamed (wote kutoka JKT Oljoro).
Cibaya aliwataja wachezaji wawili waliostaafu soka kuwa ni Hussein Bunu na Sostenesi Manyasi.
Aidha, aliwataja wachezaji askari walioachwa na kupelekwa JKT Oljoro kwa mkopo kuwa ni: Abdallah Bunu, Stanley Mkomola, Bakari Kondo, kessy Mapande Paulo Ndamko.
Cibaya aliongeza kuwa wapo wachezaji raia walioachwa na klabu hiyo ambao ni: Omary Kapilima, Kalage Mgunda, Jamal Machelanga, Emmanuel Swita, Sadick Mecky, Omary Mtaka, Stanley Mkomola, Salum Machaku na Chacha Marwa.
Kuhusu maandalizi ya msimu ujao, Cibaya alisema wanaendelea vizuri kupanga majeshi yao ili kufanya vyema tofauti na msimu uliopita.
“Sisi tunaendelea vizuri na maandalizi, kama unakumbuka hapa katikati tulikuwa na majaribio na kufanikisha kupata wachezaji mbalimbali,”

“Kwasasa tunaandaa timu ya wakubwa na wadogo. Tumefanya hivyo kama miezi mitatu au miwili na nusu. Tumepata wachezaji wadogo wazuri, kama ulikuwa unafuatilia tumefika mpaka robo fainali ya mashindano ya Rolling Stone”. Alisema Cibaya.

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog