Wednesday, August 12, 2015




SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF)  leo limesaini Mkataba wa udhamini wa miaka mitatu na mdhamini Mkuu wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, wakati maandalizi ya ligi kuu yakiendelea.
Kampuni ya Vodacom Tanzania inayoongoza hapa nchini kwa huduma za mawasiliano imekuwa mdhamini wa ligi kuu kwa miaka minane iliyopita, na sasa imeingia mkataba mpya wa udhamini kwa miaka mitatu na TFF, mkataba utakao liwezesha shirikisho hilo kupokea fedha za udhamini kwa miaka mitatu.
Ligi kuu ya Vodacom 2015/16 inayotarajiwa kaunza  katika siku za karibuni itachezwa katika viwanja mbalimbali na kushirikisha timu 16, zikiwemo timu za Mwadui na Africa Sports ambazo zimepanda daraja msimu huu. 
Rais wa TFF, Jamali Malinzi (kushoto) pamoja na Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa kampuni hiyo Kelvin Twissa (kulia) wakiwa wameshika Mkataba mpya wa udhamini wa ligi Kuu ya  Vodacom Tanzania  bara 2015/16. Anayeshuhudia (katikati) kulia ni Ofisa Mkuu Mtendaji wa bodi y Ligi, Boniface Wambura.

Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania, Kelvin Twissa (katikati) akifafanua jambo kwa waandishi wa habari(hawapo pichani) kuhusiana na mkataba mpya wa miaka(3) wa udhamini wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara uliosainiwa baina TFF na kampuni hiyo, kushoto ni Rais wa TFF, Jamali Malinzi pamoja na Ofisa Mkuu mtendaji wa Ligi, Boniface Wambura (kulia)

Mkuu wa Mawasiliano na Masoko wa kampuni hiyo Kelvin Twissa, amesema kuwa kampuni ya Vodacom iko katika mstari wa mbele katika kuunga mkono maendeleo na shughuli mbalimbali za kimichezo ndani ya nchi. 
“Wanamichezo wote ni mabalozi wazuri katika nchi. Ni wajibu wetu kuhakikisha kuwa tunawaunga mkono katika kutambua na kukuza vipaji vyao kadri tutakavyo weza,” alisema Twissa na kuongeza kuwa, “Kama jina linavyojulikana ligi kuu ya Vodacom, ligi  hii  ni maarufu nchini na nje ya nchi na inafuatiliwa na mamilioni ya washabiki wa soka nchini .”
Twissa amejivunia kampuni hiyo kuwa wadhamini wa ligi kuu kwa kipindi kingine, na kufafanua kuwa mpira wa miguu ndio unaongoza kitaifa na unapendwa na Watanzania wengi.
Mkataba huu umehusisha pande zote ambazo ni kampuni ya Vodacom Tanzania, Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na kamati ya ligi.
Kwa upande wake Rais wa TFF, Jamali Malinzi, ameipongeza kampuni ya Vodacom Tanzania akisema kuwa anaamini kuwa maendeleo ya sasa yatalenga zaidi katika kuunga mkono vipaji vipya na vilivyopo ndani ya nchi.
“Kwa niaba ya TFF, napenda kuwashukuru Vodacom Tanzania kwa kuonyesha nia na kuendelea kuunga mkono mpira wa miguu nchini. Nasi tunaahidi kuendelea kuthamini vipaji vya wachezaji wetu na kuhakikisha tunapata mafanikio zaidi,” alisema Malinzi.
MAMLAKA ya Kodi na Mapato Tanzania (TRA) inatarajiwa kuendesha semina ya kodi kwa viongozi wa vilabu viliyopo jijini Dar es salaam, siku ya ijumaa tarehe 14 Agosti katika hoteli ya Tiffany iliyopo eneo la Kisutu.
TRA itaendesha semina hiyo kwa vilabu vilivyopo ligi kuu, ligi daraja la kwanza na ligi daraja la pili ambapo viongozi wakuu wa vilabu hivyo, Katibu Mkuu, Mwenyekiti, na Mhasibu wanapaswa kuhudhuria semina hiyo.
Kwa kuanzia TRA itaendesha semina hiyo jijini Dar es salaa, na baadae kuendelea na semina hizo kwa vilabu vilivyopo mikoani kwa lengo la viongozi wa vilabu kutambua umuhimu wa ulipaji kodi kwa wachezaji, makocha wanaowaajiri katika vilabu vyao.

Semina hiyo itaanza saa 3 asubuhi mpaka saa 5 kamili asubuhi katika hoteli ya Tiffany iliyopo eneo la Kisutu jijini Dar es salaam, vionggozi wa vilabu vya ligi kuu, ligi daraja la kwanza, ligi daraja la pili waliopo jijini Dar es salaam mnaombwa kuhudhuria semina hiyo.
Timu zinazoshiriki Ligi Kuu ni Majimaji ya Ruvuma, Mbeya City, Prisons za Mbeya, Azam FC, Simba SC, Yanga SC za Dar es Salaam, Ndanda ya Mtwara, JKT Ruvu ya Pwani, Mtibwa Sugar ya Morogoro, Mgambo JKT, African Sports, Coastal Union za Tanga, Mwadui, Stand United za Shinyanga, Toto Africans ya Mwanza na Kagera Sugar ya Bukoba. 
Wakati huo huo: Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi amempongeza Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF, Adam Mambi kwa kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu nchini.Katika Salam zake kwa Jaji Mambi, Malinzi amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dokta Jakaya Kikwete kwa kumteua mwanafamilia huyo wa mpira wa miguu nchini kushika wadhifa huo.
TFF kwa niaba ya familia ya mpira wa miguu na watanzania wote inamtakia kila la kheri Jaji Adam Mambi katika majukumu yake mapya ya Ujaji katika Mahakama Kuu nchini Tanzania.
MABINGWA wa Tanzania Bara, Yanga SC wameibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Prisons jioni ya leo katika mchezo wa kirafiki Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya.
Mshambuliaji wa kimataifa wa Burundi, Amisi Joselyn Tambwe alianza kuifungia Yanga SC dakika ya tano kabla ya kutoka kipindi cha pili kumpisha Malimi Busungu aliyeingia kufunga bao la pili dakika ya 84.  
Mwinyi Hajji Mngwali wa Yanga SC na Zam Kuffoh wa Prisons, wote walitolewa kwa kadi nyekundu dakika ya 88 baada ya kupigana uwanjani. 
Malimi Busungu amefunga bao la pili leo baada ya kutokea benchi

Huo unakuwa mchezo wa pili mfululizo Yanga SC iliyoweka kambi, Tukuyu, Mbeya kujiandaa na mchezo wa Ngao ya Jamii Agosti 22, mwaka huu Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam. 
Mchezo wa kwanza Yanga SC ilicheza na Kemondo Uwanja wa CCM Viwawa, Mbozi na kushinda 4-1 mabao yake yakifungwa na Tambwe, Simon Msuva na Godfrey Mwashiuya mawili.   
Yanga SC inayofundishwa na Mholanzi, Hans van der Pluijm itashuka tena dimbani Jumapili Uwanja wa Sokoine kumenyana na Mbeya City.
Yanga SC ilikuwa ina mpango wa kumenyana na timu za Malawi na Zambia pia katika kambi yao ya huko, lakini bado haijajulikana hadi sasa kama mpango huo utafanikiwa.
Kikosi cha Yanga SC kilikuwa; Ally Mustafa ‘Barthez’, Mbuyu Twite, Mwinyi Hajji, Kevin Yondan, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Thabani Kamusoko, Simon Msuva/Deus Kaseke dk58, Haruna Niyonzima/Salum Telela dk58, Donald Ngoma, Amissi Tambwe/Malimi Busungu dk79 na Godfrey Mwashiuya/Hussein Javu dk85.

waliotembelea blog