Wednesday, July 30, 2014


Wachezaji wa Stand United (waliovalia jezi za rangi ya machungwa) wakingia uwanjani kwenye moja ya mechi ya ligi daraja la kwanza msimu uliopita
KOCHA Mkuu wa Stand United, Flugency Novatus amebwaga manyanga kuinoa klabu hiyo kuelekea msimu wa 2014/2015 wa ligi kuu soka Tanzania bara unaotarajia kuanza kushika kasi septemba 30 mwaka huu.
Akizungumza jioni hii, kocha huyo aliyeipandisha klabu hiyo ligi kuu msimu uliopita amesema sababu ya kuondoka kwake ni viongozi kushindwa kutekeleza ripoti yake iliyoiwasilisha baada ya kumalizika kwa michuano ya ligi daraja la kwanza.
“Nasikitika kukuambia kwamba kwasasa sipo Stand United. Moja ya vitu vilivyochangia ni ile hali ya kutofanyia kazi ripoti yangu. Kwahiyo niliona si busara kukaa na watu wenye mtazamo tofauti na mimi kama mwalimu.Kwasasa nimerudi Mwanza, nina karibu wiki moja sasa,” Alisema Novatus.
Novatus aliongeza kuwa yeye falsafa yake imejikita katika soka la vijana na popote anapoenda hufanya kazi kwa kusimamia misingi hiyo na kama inakuwa tofauti haoni shida kuwajibika.
“Mimi kama mwalimu nakuwa na falsafa yangu, kufanikiwa au kutofanikiwa inategemea na viongozi ulionao. Lakini kama unaona huwezi kufanikiwa kwasababu tu mtu fulani hawezi kukupa ushirikiano, sidhani kama kuna sababu ya kuendelea kuwepo,”
Aidha, Novatus aliweka wazi kuwa mkataba wake umemalizika leo juni 30, lakini hakuna mazungumzo yaliyofanyika na viongozi wa klabu hiyo inayokabiliwa na ligi ngumu yenye ushindani msimu ujao..
“Zamani ulikuwa unaweza kufanya kazi ukitegemea kuwa ipo siku mtakaa muongee, siku hizi mambo ni tofauti, mambo yanaenda kisayansi zaidi na mpira unaendelea kukua nchini kwetu. Mambo yanazidi kuwa wazi, kwasababu hata mchezaji, huwezi kumpeleka sehemu fulani akacheza bila kusaini mkataba,”
Pia kocha huyo alisisitiza kuwa maandalizi wayafanyayo Stand United haoni kama angetimiza malengo yake, hivyo njia pekee ilikuwa ni kuiacha timu na kurudi katika kituo chake cha Alliance cha Mwanza.
“Wewe kama kiongozi unajiandaaje na ligi kubwa kama hii, ligi ya Vodacom ndio ligi kubwa kuliko zote  na ndio ligi inayomtambulisha mtu. Kwasababu umeingia, muda wowote unaweza kucheza mechi za kimataifa ukishika nafasi ya kwanza au ya pili”

“Sasa kama kiongozi imejiandaa na hilo jambo?  Kama mwalimu naona taratibu hizi tunazoenda nazo hatuwezi kwenda, kuna haja gani ya kuendelea kuwepo. Kwa falsafa yangu ya vijana, nitaendelea nayo na nimerudi katika kituo changu cha Alliance cha mwanza ambapo nilitoka nikaenda Stand,” Aliongeza Novatus.

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog