Thursday, August 21, 2014


Na Baraka Mpenja, Dar es salaam
0712461976
RATIBA ya ligi kuu soka Tanzania bara msimu wa 2014/2015 unaotarajia kuanza kushika kasi septemba 20 mwaka huu ilianikwa jana na Shirikisho la Soka Tanzania, TFF.
Msimu ujao unatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa hususani kuwania ubingwa ambapo klabu za Azam fc, Yanga, Mbeya City fc, Simba, Kagera Sugar zinatabiriwa kuendelea kuwania nafasi tano za juu.
Lakini yanaweza kutokea mabadiliko kwa nafasi hizo kwasababu Mtibwa Sugar, JKT Ruvu, Coastal Union, Ruvu Shooting zinaonekana kijiandaa vizuri, hivyo timu zilizoshika nafasi tano za juu zisiwe na 100%  ya kuendelea kuwepo.
Azam fc wamekuwa na utamaduni wa kuendeleza pale walipoishia kama mambo hayatabadilika, lakini kwa Simba na Yanga wamekuwa wakipokeza nafasi za juu mara zote. Kama Simba yuko katika kiwango cha juu, basi utakuta Yanga wanasuasua, kama Yanga wako vizuri basi Simba wanakuwa ‘Mdobwedo’.
Lakini Simba na Yanga zote zinaonekana kuwa na nia ya kutwaa ubingwa msimu ujao. Zimefanya usajili mzuri wa wachezaji, lakini chachu nyingine imetokana na aina ya makocha waliopo kwa sasa.
Watakomaa msimu ujao?: Wachezaji wa Yanga wakiwa kwenye moja ya programu ya mazoezi ya Marcio Maximo.

Yanga wananolewa na Mbrazil, Marcio Maximo wakati Simba wananolewa na Mzambia mwenye historia nzuri na klabu hiyo, Patrick Phiri.
Kwa upande wa Mbeya city fc si rahisi kutabiri kwasababu wameshiriki ligi kuu kwa mara ya kwanza na kushika nafasi ya tatu, lakini ni ngumu kujua  kama wataendeleza mafanikio hayo na kupanda juu zaidi.
Historia inaonesha kuwa Tukuyu Stars iliwahi kupanda ligi kuu na kutwaa ubingwa mwaka 1986, lakini msimu uliofuata ikashuka daraja. Kwa Mbeya City hawakuweza kufikia rekodi ya kutwaa ubingwa kama ‘Banyambala’, lakini walijitahidi sana.
Kama wataendeleza pale walipoishia, basi watakuwa na uwezo wa kushika nafasi ya pili au kubeba ubingwa.
Mtandao huu utakuwa ukikuchambulia timu moja baada ya nyingine katika mechi zake kuanzia raundi ya kwanza mpaka raundi ya tisa ambapo kutakuwepo na mapumuziko ya kupisha michuano ya ‘CECAFA Seniour Challenge Cup’ na kombe la Uhai.
Leo tunaanza na wekundu wa Msimbazi Simba. Timu hii inajengwa upya baada ya kuvurunda kwa miaka mitatu mfululizo.
Kwa mara ya mwisho kutwaa ubingwa ilikuwa msimu wa 2011/2012 chini ya kocha Mserbia Milovan Circovic. Kuanzia mwaka huo imekuwa ikibadili  makocha kila wakati.
Kutoka Milovan alikuja Mfaransa, Patrick Liewig, akafuata mzawa Abdallah Kibadeni, Mcroatia Zdravko Logarusic na sasa Mzambia Patrick Phiri.
Mabadiliko ya mara kwa mara ya benchi la ufundi ni moja kati ya sababu kubwa zilizoiathiri Simba na kuondoka katika ushindani wa ubingwa kwa muda mrefu sasa.
Lakini uongozi mpya chini ya Rais, Evans Aveva umekusudia kuirudisha timu hiyo katika ushindani na kwa kuanza wameamua kumchukua kocha aliyewapa ubingwa bila kufungwa mwaka 2009, Phiri,  baada ya kuona Loga atawayeyusha msimu ujao.
Usajili waliofanya chini ya mwenyekiti wa kamati ya usajili, Keptein wa zamani wa Jeshi la Wananchi Tanzania, (JWTZ), Zacharia Hans Poppe umewapa matumaini zaidi ya kufanya vizuri.
Msimu ujao ratiba inaonesha kuwa mechi tatu za kwanza, Simba watakuwa nyumbani uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.
Raundi ya kwanza itaanza Septemba 20 mwaka huu ambapo Simba watachuana na Coastal Union.
Msimu uliopita, Simba walikuwa wazuri zaidi ya Coastal United kwa kuangalia nafasi walizoshika kwenye msimamo. Simba walishika nafasi ya nne wakati wagosi wa kaya walishika nafasi ya 9.
Kwa kuangalia takwimu hizi unaweza kusema Simba watashinda mechi, lakini Coastal wamebadilika na wanaonekana kujifua vikali ili kurudi na kasi mpya.
Kwa aina ya uchezaji wa Coastal, huwa wanawapa ugumu sana Simba katika dimba la Taifa na hata msimu uliopita walishinda bao 1-0.
Kwahiyo mechi hii itakuwa ngumu kwa Simba, lakini wana nafasi ya kushinda kutegemeana na namna Phiri atakavyokiandaa kikosi chake na utayari wa wachezaji kupambana.
Raundi ya pili ambayo itakuwa septemba 27, Simba watacheza na Polisi Morogoro uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.
Polisi Moro ni timu mpya, lakini huwezi kujua wamejipangaje msimu ujao, Wamekuwa wakiendelea kujifua kila siku, lakini ugeni wao pia utaweza kuwaathiri, ingawa imepita mwaka mmoja tu tangu washuke na kupanda tena.
Mwalimu Rishard Adolf ni mzoefu na soka la  ligi kuu na ndio maana kama unakumbuka baada ya kuichukua Polisi mwishoni mwa msimu wa 2012/2013 alijitahidi kuisogeza mbele, lakini alishuka daraja.
Mechi hii ya pili kwa Simba itakuwa ngumu, lakini wana nafasi kubwa ya kushinda kutokana na uzoefu wao.
Raundi ya tatu, Simba watakabiliana na Stand United kutoka Shinyanga,  oktoba 4 mwaka huu ndani ya uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam. Kama Stand kweli watakuja na moto waliokuja nao Mbeya City mwaka jana, mechi hii itakuwa ngumu sana kwa Simba.
Lakini kutokana na ugeni wao, kuna vitu vya kiufundi na kimbinu watazidiwa na Simba yenye wachezaji mchanganyiko. Lakini mpira una vitu vingi, wanaweza kushinda, ila nadhani Simba watakuwa kwenye nafasi kubwa ya kushinda kutokana na mazingira ya uwanja wa Taifa ambao utaweza kuwaduwaza baadhi ya wachezaji wa Stand.
Baada ya kucheza mechi hizo tatu, raundi ya nne Oktoba 4 mwaka huu uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam, Simba watakuwa wageni wa Yanga ya Marcio Maximo.
Hii itakuwa mechi ngumu kwa pande zote. Simba na Yanga mechi zao hazitabiriki kirahisi. Timu bora inaweza kupoteza mechi au kushinda.
Usitumie kigezo cha Yanga kuwa bora zaidi ya Simba au simba kuwa bora zaidi ya Yanga na kutabiri timu fulani kushinda, wakati fulani hesabu kama hizi huwa hazifanyi kazi inapofika mechi ya watani wa jadi.
Hata msimu uliopita ambao Yanga walikuwa wazuri zaidi ya Simba, walishindwa kupata matokeo mechi ya mbili za ligi kuu ambapo mzunguko wa kwanza walitoka sare ya mabao 3-3 na mechi ya marudiano walitoka sare ya 1-1.
Wengi walijua Yanga wanashinda kutokana na namna walivyosheheni nyota wengi tofauti na Simba, lakini Mnyama aligoma kuvutwa sharubu na la kukumbuka zaidi ni jinsi alivyoweza kumcharaza Yanga kwenye mechi ya Nani Mtani Jembe ambapo alishinda 3-1 mwezi desemba mwaka jana.
Baada ya kibarua na Yanga, raundi ya tano itakuwa Oktoba 5, Simba watasafiri mpaka Mbeya kucheza mechi yao ya pili ugenini dhidi ya Tanzania Prisons uwanja wa sokoine jijini humo, lakini itakuwa kama ya kwanza kwasababu moja watakuwa wamecheza Taifa.
Sokoine ni miongoni mwa viwanja ambavyo si rafiki kwa Simba. Simba wamekuwa wakihenyeka mno kupata ushindi mbele ya Prisons.
Licha ya Prisons kutokuwa katika ubora wake, mechi hii itakuwa ngumu na nadhani sare ndio matokeo nanayoanza kutabiri, lakini mabao pia yataweza kupatikana kwa timu yoyote.
Raundi ya sita Oktoba 26, Simba watakuwa uwanja wa Jamhuri Mjini Morogoro kucheza na Mtibwa Sugar. Hii itakuwa mechi ngumu kwa Simba na siwapi nafasi ya kushinda mbele ya wakata miwa, zaidi naamini sare ndio yatakuwa matokeo rafiki kwa Simba.
Raundi ya saba itakuwa Novemba 2 ambapo Simba watarudi nyumbani uwanja wa Taifa kukipiga na Ruvu Shooting. Hii itakuwa mechi nyingine ngumu kwa Simba kutokana na Shooting kuendelea kubadilika.
Lakini kutokana na namna Shooting wanavyocheza wakiwa uwanja wa Taifa ambapo hawaoneshi makali sana, nadhani Simba wataweza kufanya vizuri ingawa sio lazima iwe hivyo.
Raundi ya nane, Novemba 8, Simba watacheza tena uwanja wa Taifa dhidi ya Kagera Sugar. Hii itakuwa mechi ngumu sana kwa Simba kutokana na uwezo mkubwa ambao huoneshwa na timu hii ya Kaitaba inapocheza uwanja wa Taifa.
Raundi ya tisa itakuwa Novemba 16 ambapo Simba watacheza ugenini dhidi ya  Mgambo JKT katika uwanja wa CCM mkwakwani.
Kwa kuangalia namna Mgambo walivyotumia uwanja wa Mkwakwani hasa mechi za mzunguko wa pili msimu uliopita, unapata picha kuwa Simba watahitaji kujipanga zaidi.
Baada ya raundi ya tisa kutakuwa na mapumziko ya kombe la mataifa ya Afrika mashariki na kati na kombe la Uhai.
Mpaka kufikia raundi hiyo, Simba watakuwa wamecheza mechi tano nyumbani. Lakini unaweza kusema sita kwasababu mechi na Yanga itapigwa uwanja wa Taifa ambao unatumika na klabu hizo mbili kama uwanja wa nyumbani.
Kwa mazingira haya, kama Simba watatumia vizuri uwanja wa nyumbani watakuwa wamekaa nafasi nzuri katika msimamo, lakini mpira imebadilika, unaweza kufungwa kote kote.
Kesho tutaiangazia Yanga. Nawatakia siku mwema!

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog