Thursday, March 13, 2014

Pix-1_1ee2f.jpg
Mtendaji Mkuu Bodi ya Filamu, Bi. Joyce Fisoo akiwasilisha Rasimu ya awali ya Sera ya Filamu wakati wa moja ya kikao cha wadau cha kujadili rasimu ya awali ya Sera ya Filamu kilichofanyika hivi karibuni. Kulia ni Mkurugenzi msaidizi kutoka Idara ya Sera na Mipango Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Bi. Verediana Mushi, na Kushoto ni mdau wa filamu Bw. John Kitime.
Pix-2_12697.jpg
Baadhi ya wadau mbalimbali wa tasnia ya filamu wakijadiliana wakati wa kikao cha wadau cha kujadili rasimu ya awali ya Sera ya Filamu kilichofanyika hivi karibuni.
SERIKALI ya Tanzania imejipanga kuendeleza kwa dhati tasnia ya filamu nchini ili kuwa chanzo kikubwa cha ajira kwa wasanii na pia kuongeza uchumi wa nchi. Ni dhahiri kuwa sekta ya filamu ni njia madhubuti ya kutambulisha jamii kiutamaduni, kisiasa na kijamii na pia katika kukuza na kuongeza fursa za nchi katika uwekezaji na utalii.
Filamu na makala za filamu zikitumika vizuri zitaweza kuhamisha na kuondoa tofauti mbalimbali zilizopo ndani ya jamii na hivyo kuongeza umoja na mshikamano baina ya watu wa makabila na watu wenye asili mbalimbali, hivyo kuutambulisha utamaduni wa Mtanzania. Kazi na shughuli za Filamu nchini zimekuwa zikisimamiwa na Sera ya Utamaduni ambayo ilitayarishwa na kupitishwa mwaka 1997 pamoja na Sheria ya Filamu na Michezo ya Kuigiza na 4 ya mwaka 1976.
Katika kipindi cha kuanzia mwaka 1997 hadi mwaka 2013 kumekuwepo na maendeleo makubwa katika Tasnia ya Filamu nchini hivyo kuisababishia Sera ya Utamaduni ya Mwaka 1997 kutokidhi baadhi ya mahitaji ya tasnia ya filamu na kupelekea mahitaji ya kurekebisha Sera ya Utamaduni kama Sera mama na kutungwa kwa Sera ya Filamu.
Mnamo Desemba 12 mwaka 2013, wadau mbalimbali kutoka Wizara ya Habari, Vijana Utamaduni na Michezo, Bodi ya Filamu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi walishiriki katika kikao cha wadau cha kujadili rasimu ya awali ya Sera ya Filamu.
Wadau wengine ni Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Wizara ya Kazi na Ajira, BASATA, Idara ya Sanaa na Sanaa za Maonesho, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Mamlaka ya Mapato Tanzania, Mtandao wa Muziki, Swahili Films, ROSAF, TAPAF, Umoja wa Mashirikiano wa Filamu, Filamu Cental, Chama cha Hakimiliki Tanzania, Shirikisho la Sanaa za Maonyesho pamoja na G&S Associates and Advocates.
Wizara inapenda kuujulisha umma kuwa imekua na inaendelea kushirikiana na wadau wa Filamu kwa kila hatua ili hatimaye ifanikishe azma ya kuwa na nyaraka zote muhimu katika kuendeleza, kusimamia, kuratibu na kukuza tasnia ya filamu nchini.

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog