Saturday, February 8, 2014

mnyikaclip1 2616f
Mbunge wa Ubungo, Dar es Salaam, John Mnyika amependekeza kusitishwa kwa muda kwa uwindaji wa tembo nchini kama njia muhimu ya kupambana na vitendo vya ujangili.
Mnyika ambaye alikuwa akizungumza kama Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, alitoa mapendekezo hayo juzi baada ya kutembelea Hifadhi ya Tarangire.
"Tatizo hili (la ujangili) ni kubwa ni vizuri Tanzania ikaiga nchi nyingine duniani...Tupige marufuku kwanza kwa muda uwindaji wa tembo ili kuziba kabisa mianya na visingizio," alisisitiza Mnyika.
Mnyika amewaambia waandishi wa habari kuwa, kwa hali ilivyo sasa, wapo tembo wanaowindwa kwenye vitalu na hiyo inaleta mkanganyiko kati ya uwindaji haramu na uwindaji halali.
Halikadhalika Mnyika ametumia fursa hiyo kuitaka Serikali kuwataja na kuwashtaki kortini vigogo wa ujangili kabla ya kuanza kwa awamu ya pili ya Operesheni Tokomeza Ujangili (OTU II).
"Kabla ya kuanza kwa awamu ya pili ni vizuri wale vigogo wa ujangili waliotajwa kwa ujangili wakatajwa kwa majina ili wachukuliwe hatua...Tunataka itakapoanza awamu ya pili isiwalenge tu wananchi," alisema Mnyika.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, James Lembeli alisema, wanyama kama Nyumbu wapo hatarini kutoweka kama hatua za makusudi hazitachukuliwa.
Amesema kutoweka kwa wanyama hao kutasababishwa na wimbi kubwa la kuzibwa kwa mapito ya wanyama (corridor) kati ya hifadhi na hifadhi na hivyo wanyama hao kushindwa kwenda kuzaliana.
"Hali hii ni hatari kwa maisha ya hifadhi zetu hasa hizi za kaskazini...Mfano wakati hii Tarangire inaanzishwa kulikuwa na Corridor (mapito) tisa, leo tunapozungumza zimebaki tatu tu,"alisema.
Lembeli amesema endapo ikitokea njia hizo zikazibwa kabisa, wanyama watajikuta wanabakia eneo moja na kushindwa kwenda maeneo ya kuzaliana, hivyo watazeeka na kufa bila kuongezeka. Chanzo: mwananchi

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog