Tuesday, July 22, 2014


legends_of_real_madrid_david_beckham_ronaldo_raul_real_madrid
Na Baraka Mpenja, Dar es salaam

WAZEE wa kale walishasema, `Bahati haiji mara mbili`!. Kumekucha kwa Watanzania kuwaona `laivu` magwiji waliotikisha soka la dunia ngazi ya klabu na michuano ya kimataifa ikiwemo kombe la dunia.
Magwiji waliocheza kwa mafanikio makubwa katika klabu ya Real Madrid wanatarajia kufanya ziara ya siku nne nchini kuanzia Agosti 22 mwaka huu ambapo watacheza mechi moja ya kirafiki dhidi ya kikosi maalum cha nyota wa Tanzania.
Ziara hiyo ni mwaliko wa kampuni ya Tanzania Sisi ni Nyumbani (TSN), chini ya mkurugenzi wake mkuu, Farough Baghozah na meneja wa ziara hiyo ni Dennis Ssebo.
Akizungumza na mtandao huu mchana wa leo, Dennis Ssebo amesema maandalizi ya ziara hiyo yanakwenda vizuri na watanzania watarajie kuwaona wachezaji wakubwa waliotamba miaka ya nyuma kama vile Ronaldo Delima, Luis Figo, Roberto Carlos, Zinedine Zidane na wengineo.
“Ninaloweza Kusema ni kwamba,  Watanzania wakae tayari kupokea wachezaji 27 wa zamani wa timu ya Real Madrid na mashabiki 23  kutoka Hispania wanaokuja kuwashangilia magwiji wao. Kwahiyo jumla tunapokea watu 50 kutoka Hispania kwa ajili ya ziara hii”. Alisema Ssebo.
“Ni ziara ambayo tulifikiria itakuwa fupi, lakini wenzetu kumbe wameipenda nchi na wanaifahamu, kwahiyo ni ziara ambayo itachukua takribani siku nne”. Aliongeza.
Ssebo alisema Magwiji hao wataingia nchini Agosti 22 mwaka huu na watacheza mechi maalumu ya kirafiki Agosti 23 ndani ya dimba la kisasa la Taifa, jijini Dar es salaam.
“Baada ya mechi wataenda Arusha Agosti 25 kuangalia vivutio vya utalii na watalala huko. Watalala tena Dar es salaam na kuondoka tarehe 26 ya mwezi wa nane”.
“Kwahiyo ni ziara ambayo ni ndefu kidogo, watu ni wengi, tulifikiri timu ingekuja peke yake, kumbe kuna mashabiki wanaotoka Hispania kuwashangilia hao magwiji, nafakiri Watanzania tukae mkao wa kula,”. Alifafanua Ssebo.
Kuhusu viingilio vya mechi hiyo, Ssebo alisema watakuwa na kiwango cha chini kinachoweza kulipwa na watanzania wengi.
“Tunawahakikishia watanzania kuwa wataangalia mechi hii kwa kiwango cha chini kabisa.”
“Naweza kuthubutu kusema kuwa kiwango cha chini kabisa kitakuwa shilingi elfu 5 ambacho tunaamini Watanzania wa kawaida wataipata kwasababu tumewaambia mapema kwa mwezi mzima.” Ssebo alisema.
 “ Lakini kikubwa zaidi, ni kuwahakikishia watanzania kuwa ziara hii itafungua milango ya kujiuza na kuuza vivutio vyetu vya utalii”.
“ kwahiyo ni zaidi ya mpira na sisi tunaamini kabisa kuwa tutakuwa na uwezo wa kuuza vitu vyetu, kwasababu wao watakuja na mashabiki, halafu Real Madrid TV watakuja kurekodi ziara nzima timu ikiwa Tanzania”. Alisema Ssebo.

Hii ni ziara ya kwanza kabisa kwa klabu ya Real Madrid kufanya barani Afrika, hivyo ni bahati kwa Tanzania kuwa nchi ya kwanza kutembelewa na timu kubwa ya Real Madrid.

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog