Thursday, May 8, 2014

PLUIJMKITAMBI


SAM_2259 Aliyekuwa Kocha mkuu wa Yanga sc, Hans Van Der Pluijm ( wa kwanza kulia) akiwa na wasaidizi wake, Boniface Mkwasa ( wa pili kulia) na Juma Pondamali ( wa tatu kulia)

KOCHA  mkuu wa Young Africans, Mholanzi, Hans Van der Pluijm amepata kazi mpya nchini Saudi Arabia na tayari ameshaaga rasmi mchana huu kwa wachezaji wake, viongozi, wapenzi na wanachama wa klabu hiyo.
Pluijm aliyejiunga na Yanga mapema januari mwaka huu umepata shavu hilo katika klabu ya Al Shoalah FC inayoshiriki ligi kuu soka nchini Saudi Arabia.
Mholanzi huyo amemaliza mkataba wake wa miezi sita na klabu ya Yanga, lakini mbaya zaidi ameshindwa kuwasaidia wanajangwani kutetea ubingwa wao msimu huu uliomalizika aprili 19 mwaka huu. 
Yanga chini ya Pluijm ilimaliza katika nafasi ya pili, huku Azam fc chini ya kocha Mcameroon, Joseph Marius Omog wakibeba taji lao la kwanza tangu wapande ligi kuu msimu wa 2008/2009. 
Pluijm alirithi mikoba ya mholanzi mwenzake, Ernie Brandts aliyetimuliwa mwezi desemba mwaka jana baada ya kufungwa mabao 3-1 na Simba katika mechi ya Nani Mtani Jembe.
Brandts aliondoka pamoja na wasaidizi wake Fredy Felix Minziro na kocha wa makipa Mkenya Razak Ssiwa na nafasi zao kuchukuliwa  na Pluijm, Charles Boniface Mkwasa na Juma Pondamali `Mensah`.
Taarifa rasmi kutoka Yanga inaeleza kuwa Pluijm aliyeiongoza Yanga kwa miezi mitano imesema  kuwa Puijm ametoa shukurani zake kwa ushirikiano  mkubwa aliokuwa anapewa kwa kipindi chote alichokaa na Yanga.
Pluijm amekaririwa akisema: "Najua wengi itawashangaza kuona naondoka,  lakini ukweli ni kwamba nilikua na hii dili hata kabla ya kuja Yanga”.
“ Nilikuwa na makubaliano na timu ya Al Shoalah FC, ambayo yanaanza mwezi ujao, hivyo nilikubaliana na viongozi wa Yanga kuja kufanya kazi kwa kipindi cha miezi sita tu”.
“Nashukuru tumefanya kazi salama na baada ya mkataba huo kumalizika nipo tayari kurudi kuja kufanya kazi Tanzania" alisema Pluijm.
Aidha , Pluijm alieleza kuwa tayari ameshajaza fomu ya uanachama wa Yanga,  hivyo anajiona ni sehemu ya klabu hiyo yenye makazi yake makutano ya Twiga na Jangwani, Kariokoo,  jijini Dar es salaam.
Kocha huyo aliongeza kuwa yupo tayari kuisaidia Yanga kupata wachezaji wazuri watakaoisaidia klabu katika michuano ya ligi kuu soka Tanzania bara msimu ujao na michuano ya kombe la shirikisho.
Pluijm anaondoka leo nchini kwenda Ghana kisha atakwea pipa kwenda nchini Saudi Arabia tayari kwa kujiandaa na maandalizi ya msimu ujao wa ligi kuu nchini humo.
Mkataba wa Pluijm na klabu hiyo ya Saudia ni wa mwaka mmoja.
Tayari  kocha huyo ameshakabithi ripoti jana, kinachofuata ni viongzoi kuifanyia kazi na baadaye kuweka wazi nini mapendekezo yake.

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog