Sunday, July 12, 2015



NIPASHE
Mgombea wa kiti cha urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM) na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe ‘amefunguka’ baada ya kupenya katika kundi la tano bora, akisema iwapo wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), hawatamuunga mkono, yupo tayari kuheshimu maamuzi yao.
Membe na makada wenzake, Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli, Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Asha Rose Migiro, Naibu Waziri wa Sayansi, Mawasiliano na Teknolojia, January Makamba, Balozi wa Kudumu wa Umoja wa Afrika (AU), nchini Marekani, Amina Salum Ali, ndio waliopeta kati ya wagombea 38 waliorejesha fomu, wakiomba kuteuliwa na chama hicho kupeperusha bendera katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 25, mwaka huu.
“Hata kama sitachaguliwa na wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Taifa, kuwa mgombea wa CCM katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu, nitamuunga mkono atakayechaguliwa. Kukubali kushindwa ni sehemu ya demokrasia na mimi nimejiandaa kisaikolojia kupokea matokeo yoyote…Lakini pia niwapongeze wote waliofika tano bora,”  Membe.
Mgombea mwingine, Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli alipoulizwa kuhusu mapendekezo ya Kamati Kuu (CC) kuliteua jina lake kuwa miongoni mwa majina matano yatakayopigiwa kura ili kupata majina matatu yatakayopigiwa kura ili kumpata mgombea mmoja atakayepeperusha bendera yake dhidi ya vyama vya upinzani, alikataa kuzungumza huku akiwapungia mkono wananchi waliojitokeza eneo hilo.
Naye, Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Asha-rose Migiro akizungumzia mchakato huo namna ulivyokwenda licha ya kuwapo kwa mpasuko kati ya baadhi ya wajumbe wa Kamati Kuu ambao wanapinga maamuzi ya kuminya wagombea wanaokubalika ndani na nje ya CCM akiwamo Lowassa, Migiro alisema  kitendo cha kuaminiwa na CCM, hadi kufika hatua ya tano bora, ni unyenyekevu uliopitiliza ambao unapaswa kuheshimiwa.”
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Sayansi, Mawasilino na Teknolojia, January Makamba, alisema “Tayari chama changu kinaamini kuwa mimi ninaweza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania…kwa hiyo kwangu mimi ni heshima kubwa sana.”
Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja ambaye ni miongoni mwa wagombea walioshindwa kupenya tabo bora, alisema kuwa kilichofanywa na Kamati Kuu ya CCM; ni utaratibu wa kawaida ambao vyama vilivyokomaa kidemokrasia vimekuwa vikiufuata.
“Mimi binafsi naafiki kuwa kilichofanyika ni utaratibu wa kawaida ambao hufuatwa na chama change. Wametenda haki wajumbe wa Kamati Kuu lakini pia nakubaliana nao kwamba, wagombea wote waliochaguliwa wana uwezo wa kuliongoza taifa hivyo sina wasiwasi nao,”
NIPASHE
Watu wasiofahamika wamesambaza vipeperushi Zanzibar kupinga maamuzi ya Kamati Kuu ya CCM kuwakataa wanasiasa wakongwe waliojitokeza kuwania nafasi ya urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwemo Makamu wa Rais, Dk. Mohammed Gharib Bilali na Waziri mkuu wa zamani Edward Lowassa.
Vipeperushi hivyo vyenye kurasa mbili vimeonekana katika maeneo tofauti vikiwa na kichwa cha habari “Sauti ya salama Zanzibar”, vimeeleza kuwa kutokana na maamuzi hayo wanachama wa CCM wa kundi la sauti ya salama kuanzia leo ndio mwisho wa wanachama wa sauti ya salama kuendelea kubakia ndani ya CCM.
Walisema kundi hilo linaundwa na mikoa sita ya kichama, wamefikia uamuzi huo baada ya kuridhishwa na utaratibu mzima wa upatikanaji wa mgombea wa nafasi ya urais kutokana na chama kushindwa kupitisha mgombea ambaye ni chaguo la wananchi na wanachama.
“Kama mtatuletea mgombea wenu wa mfukoni badala ya Lowassa ambaye ndio chaguo la wanachama wengi na wananchi, Jumapili ndio mwisho kwa wanachama wa sauti ya salama kuendelea kubakia ndani ya CCM”, vimeonya vipeperushi hivyo.
Aidha, kundi hilo limesema wajumbe wa halmashauri kuu ndio wanaowategemewa na kama watashindwa kukiokoa chama kwa kushindwa kuwapatia wanachotaka, wanachama historia itakuja kuwahukumu kama ilivyotokea kwa vyama vya ukombozi katika mataifa ya Malawi, Zambia na Kenya baada ya vyama husika kushindwa kuheshimu demokrasia ya ndani ya chama.
Kundi hilo limesema kuwa kumbukumbu inaonyesha mchakato wa kupata mgombea wa urais CCM umekuwa ukimalizika na kuacha nyufa ndani ya chama kama ilivyotokea mwaka 2000 baada ya wananchama na wananchi wa Zanzibar kumtaka aliyekuwa Waziri Kiongozi, Dk. Mohammed Gharibu Bilali awe mrithi wa rais mstaafu Dk Salmin Amour, baada ya kumaliza muda wake.
Vipeperushi hivyo ambavyo vimeibua mjadala vimeeleza kwamba mwaka 2010 chama kiliendelea kurejea makosa yale yale kuchagua mgombea wa mfukoni badala ya yule aliyetakiwa na wananchi ambao walikuwa wakimtaka Dk. Bilal na badala yake aliletwa mgombea Dk Ali Mohammed Shein na kusababisha CCM kushinda kwa asilimia 51.
“Kamati kuu, halmashauri kuu pamoja na mkutano mkuu kama utashindwa kusoma alama za nyakati tutalazimika wanachama kupita njia yenye usalama na miguu yetu, kumbukeni vipo vyama vingi na tayari Chadema imetuonesha njia”.
Hata hivyo wasemaji wa CCM hawakuweza kupatikana kutokana na kuhudhuria vikao vya chama Dodoma akiwemo Naibu Katibu mkuu wa CCM, Vuai Ali Vuai, lakini Kamanda wa polisi mkoa wa mjini Magharibi Mkadam Khamis Mkadam, alisema hadi jana hajapokea taarifa ya kusambazwa vipeperushi vinavyopinga maamuzi yanayoendelea kutumika ya kupata mgombea wa urais.
NIPASHE
Wachambuzi wa masuala ya kisiasa wamesema kuwa kitendo cha makada watatu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Mjumbe wa Kamati Kuu, Dk. Emmanuel Nchimbi, Sophia Simba na Adamu Kimbisa, kueleza kuwa, hawakubaliani na maamuzi yaliyofanywa na Kamati Kuu ni kiashirio kuwa, CCM imeyumba na inampasuko ndani yake.
Mchambuzi wa Siasa na Uongozi, Rutashobya Rutashobya, akizungumza na NIPASHE Jumapili jana alisema kuwa kitendo cha makada hao juzi usiku kuibuka na kauli moja kuwa, hawakubaliani na maamuzi yaliyofanyika maana yake wamekosa umuvilivu wa kisiasa na kusababisha chama kuyumba.
Juzi makada hao baada ya kumalizika kwa kikao cha Kamati Kuu, waliwaeleza waandishi wa habari kuwa, hawakubaliani na maamuzi yaliyofanywa na kikao hicho ya kuminya baadhi ya majina ya wagombea.
Aidha, walisema kuwa wameletewa majina machache yaliyojadiliwa na Kamati ya Maadili, kitendo ambacho hawakukubaliana nacho kwa mujibu wa Katiba ya chama.
Nchimbi na wenzake walisema tayari wameshawataarifu wenzao kuhusiana na maamuzi yaliyofanywa na Kamati Kuu ya kutounga mkono kile kilichotokea.
Akizungumzia maamuzi hayo, Rutashobya, alisema , makada hao walitakiwa kuwa na uvumilivu wa kisiasa lakini walichokifanya inaonyesha dhahiri kuwa kuna mpasuko na chama kimeyumba.
Aidha, alisema kwa wale walioenguliwa kwa bahati mbaya sababu hazijawekwa wazi hivyo ni vigumu kama wachambuzi kuchambua kitaalam.
Aidha alisema bado wananchi wana nafasi kubwa ya kuchagua Rais ajae.
Akielezea kuhusu kuenguliwa kwa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, ambaye mikutano yake wakati akitafuta udhamini ilifurika wananchi, alisema inawezekana waliokuwa wakijitokeza walikuwa wanapenda kitu kingine cha ziada na sio mhusika.
“Mtu aliyekuwa anajaza umati mkubwa uwanjani leo ameenguliwa lakini nchi ipo shwari hakuna aliyeenda barabarani kufanya maandamano kupinga maamuzi, ni tafsiri kuwa labda umati ule ulikuwa ukienda pale kushangaa waimbaji, magari na sio upendo wa dhati kwa mhusika,” alisema.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam (UDSM) Bashiru Ally, alisema kama mchambuzi wa siasa, kilichotokea na kitachotokea atakichambua kwa kina kwa faida ya Watanzania.
Alisema endapo leo jina la mgombea litatoka basi atakuwa na uwanja mpana wa kuchambua mchakato mzima kutoka watia nia 42 hadi wakabaki 38 na mwishoe watano.
Kuhusu kuenguliwa kwa Lowassa na watia nia wengine alisema anaamini maswali yanayoulizwa nje na wananchi hata ndani ya vikao yapo.
“Huu ni mwanzo tu kwa yaliyotokea nafikiri yapo matokeo kama 1000 yataweza kutokea lakini sasa ni mapema mno kuchambua tuvute subira hadi jina la mgombea urais litakapotoka,” alisema.
Mhadhiri Mwandamizi wa Idara ya Sayansi ya Siasa na Utawala wa Umma,  Alexander Makulilo,  alisema kilichotokea kwa CCM inaonyesha kuwa, kuna shida labda Kamati ya Maadili ilipeleka Kamati Kuu majina kama muhuri wa kupitishwa majina badala ya kufanyiwa kazi.
Akitoa maoni kuhusu tano bora, alisema miongoni mwao atakayechaguliwa akipata mfumo mzuri wa  uongozi mambo yataenda vizuri.
Mhadhiri wa Chuo kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Benson Bana, alisema kuenguliwa kwa mtu ambaye alikuwa anaonekana ana nguvu kubwa kwa wananchi ni kiashirio tosha kuwa kazi ndani ya CCM haikufanyika kwa vigezo.
kadhalika kuhusu kitendo cha baadhi ya makada kutangaza kuwa hawana imani na kilichotokea, alisema  “Hata kama walifanya mchujo huu naamini CCM ina watu wenye busara na hekima kwa hiyo walipaswa  kuwa na maridhiano,” alisema.
Aliongeza kuwa kiashiria cha kilichotokea ni kwamba uchaguzi mkuu utakuwa na makundi yanayopingana ndani ya chama na kuleta fursa kwa upinzani.
Alisema kuwa inapotokea chama kinamkataa mgombea mwenye watu wengi nje anaweza kwenda upinzani na kuzigawa kura.
Aidha, alikitaka chama tawala kujitathmini upya kupitia  kile kilichotokea cha baadhi ya wajumbe kupinga maamuzi.
“CCM iangalie upya kanuni zake ili hapo baadaye watu waweze kuhoji maamuzi inapobidi,” alisema.
MWANANCHI
Sasa ni wazi; mmoja kati ya Dk John Magufuli, Dk Asha Rose Migiro au Balozi Amina Salum Ali atapeperusha bendera ya CCM kwenye Uchaguzi Mkuu ujao baada ya wajumbe wa Mkutano Mkuu kukamilisha kazi yao ya kupiga kura usiku mwingi wa kumkia leo.
Licha ya mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete kutangaza kuwa matokeo ya kura hizo yatatangazwa leo saa 4:00 asubuhi kuna kila dalili kuwa Waziri wa Ujenzi, Dk Magufuli ndiye atakayepeperusha bendera ya chama hicho.
Lakini ushindi wa Dk Magufuli unakabiliwa kikwazo kikubwa kutoka kwa makada hao wawili wanawake na wanadiplomasia.
Watatu hao walifanikiwa kuingia hatua hiyo ya mwisho ya kupigiwa kura na mkutano mkuu baada ya kuwabwaga makada wengine wawili, Bernard Membe, ambaye alikuwa akipewa nafasi kubwa kutokana na Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa kuenguliwa na Kamati Kuu juzi, na January Makamba katika kura zilizopigwa na wajumbe wa Halmashauri Kuu.
Awali kabla ya kupigiwa kura na Mkutano Mkuu jana, Kikwete aliwataka wajumbe kumuunga mkono mgombea atakayepitishwa kupeperusha bendera ya chama hicho na kuachana na makundi.
“Wagombea wapo watatu na wote wana sifa za kuwa Rais. Halmashauri Kuu imewapitisha kwa kujiridhisha na tabia na mienendo yao na atakayepitishwa ataiongoza nchi yetu vizuri. Anatakiwa apatikane Rais zaidi yangu ili tusonge mbele. Tunataka rais atakayefanya mambo zaidi yangu,” alisema JK.
“Tumevuka hatua ya makundi na sasa tunatafuta mgombea wa chama na si mgombea wa kundi au mgombea binafsi. Wagombea urais waliojitokeza walikuwa 38 na makundi lazima yalikuwa mengi. Tukipata mgombea mmoja makundi yanatakiwa kuyeyuka.”
Hisia za wajumbe kwa Dk Magufuli zilionekana wazi wakati makada hao walipopewa dakika 15 za kujieleza mbele ya Mkutano Mkuu, huku mwenyekiti akiweka sharti la kuzuia kushangilia hata kama wakiguswa. Lakini sharti hilo lilionekana kuwasumbua wajumbe hao na mara kwa mara wakajikuta wakilipuka na kushangilia.
Akijinadi kwenye mkutano huo, Dk Magufuli, ambaye alizungumza kwa dakika tisa kuanzia saa 5:55 hadi saa 6:04 usiku, aliwashukuru wajumbe wa mkutano huo, wakiwamo wageni waalikwa na muda huo wajumbe wakaanza kumshangilia.
“Naombeni kura kwa sababu ninaamini kuwa nitafanya kazi na nyinyi na mtanituma na nitakuwa mwakilishi wenu na nitailinda CCM katika kushinda kikamilifu na kushika dola ili kuiongoza nchi hii. Nitadumisha Muungano wetu,” alisema Magufuli.
“CCM imenilea na ninawaahidi wajumbe sitawaangusha. Nimefanya kazi na Rais Kikwete na nadhani sikukuangusha. Umenituma katika kipindi chote cha miaka 10 na nilidhani leo utataka nielezee bar
MWANANCHI
Marais wastaafu watatu na makamu wa zamani wa CCM jana walifanya kazi kubwa ya kukinusuru chama hicho kuingia kwenye mgogoro uliokuwa unanukia baada ya Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa kuenguliwa kwenye mbio za urais.
Kwa mara ya kwanza, wajumbe watatu wa Kamati Kuu ya chama hicho juzi walijitokeza hadharani na kupinga uamuzi wa chombo hicho wa kupitisha majina ya wagombea kwa njia ambazo walisema zinazokiuka katiba ya CCM.
Kama hiyo haitoshi, jana wajumbe wa Halmashauri Kuu walimuweka mwenyekiti wao, Rais Jakaya Kikwete kwenye hali ngumu baada ya kuimba wimbo wa kuonyesha kuwa na imani na Lowassa, likiwa ni tukio la kwanza la aina yake kwenye vikao vya juu vya chama na ambalo liliashiria kuanza kupoteza utii kwa chama.
Habari kutoka ndani ya NEC zinasema kuwa baada ya mapumziko ya chakula cha mchana, kikao hicho kilijadili kwa kirefu sakata la kuchujwa kwa Lowassa na pande zinazohusika zilizungumza kwa hisia kali, ndipo marais hao, Benjamin Mkapa, Ali Hassan Mwinyi, Abeid Amani Karume na makamu mwenyekiti wa zamani, John Samuel Malecela walipolazimika kuingilia kati.
“Ilibidi kwanza wote waliokuwa wanagombea urais waondolewe kwenye mkutano ndipo tuanze kujadiliana,” alisema mmoja wa wagombea ambaye aliomba jina lake lihifadhiwe.
Mjumbe mwingine wa kikao hicho alisema Malecela, Mkapa, Karume na Mwinyi walitumia maneno ya busara na kuwatahadharisha wajumbe dhidi ya misimamo yao.
“Walituonya kuhusu kujali masuala yetu binafsi kuliko amani ya nchi na kututaka kuangalia sana misimamo yetu kwa kuwa inaweza kuhatarisha amani,” alisema mjumbe huyo.
Alisema wakati kikao kilipositishwa kwa ajili ya chakula cha mchana, kuna baadhi ya wajumbe waliondoka eneo hilo na wengine kubaki, akiwamo Lowassa ambaye hakujulikana alielekea eneo gani kwenye jengo hilo.
Kikao cha mchana kilianza bila ya Lowassa kuwamo na Karume alianza kuzungumza, na kufuatiwa na Malecela, Mkapa, na Mwinyi, ambaye alipomaliza aliwashauri wajumbe kuwa waendelee na upigaji kura kwa kuwa suala hilo limeshaeleweka.
Mkutano ulipoanza kupiga kura ndipo Lowassa alipoingia na kukuta kazi ya upigaji kura inaendelea na hivyo kuendelea na shughuli hiyo.
Awali, kwa mara ya kwanza, Kikwete jana alikumbana na mapokezi ya aina yake wakati wajumbe walipomuonyesha waziwazi kupinga uamuzi wa Kamati Kuu kwa kuimba wimbo wa kumuunga mkono Edward Lowassa kabla ya kikao cha Halmashauri Kuu kuanza.
Hali hiyo imetokea wakati baadhi ya wanachama wa CCM wakiwa bado hawajakubali kuenguliwa kwa Lowassa kwenye kinyang’anyiro cha urais kwa tiketi ya CCM baada ya Kamati Kuu kupitisha majina ya John Pombe Magufuli, Amina Salum Ali, Bernard Membe, January Makamba na Dk Asha Rose Migiro kwa ajili ya kupigiwa kura Halmashauri Kuu.
HABARILEO
Zoezi la uboreshaji daftari la kudumu la wapiga kura kwa mkoa wa Dar es Salaam limesogezwa mbele hadi Julai 22 mwaka huu.
Uamuzi huo umetokana na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kupokea maombi kutoka kwa wadau mbalimbali walioomba tarehe ya kuanza uandikishaji iliyopangwa kufanyika kuanzia Julai 16 iahirishwe ili kupisha sherehe za Eid-El-Fitr ambazo zinatarajiwa kufanyika kuanzia tarehe hizo.
Taarifa iliyotolewa na Tume ilisema kuwa kwa kuzingatia umuhimu wa sherehe ya waumini wa dini ya Kiislamu pamoja na watu wengine Tume imeamua kusogeza tarehe ya kuanza kwa uboreshaji wa daftari hilo hadi Julai 22.
“Tume imezingatia kwa uzito maombi yaliyotolewa na wadau mbalimbali kuhusu kusogezwa mbele tarehe ya uandikishaji uliotakiwa kuanza Julai 16 na badala yake kazi hiyo itaanza rasmi Julai 22 hadi 31 mwaka huu,” ilisomeka taarifa hiyo.
Kwa mujibu wa Tume hiyo, uandikishaji unawahusu wananchi wa mkoa wa Dar es Salaam pamoja na wananchi wa kata ya Bunju na Mbweni waliojiandikisha wakati wa majaribio.
Aidha Tume inatoa wito kwa wananchi wote wa mkoa wa Dar es Salaam kujitokeza kwa wingi kujiandikisha ili wasipoteze haki yao ya msingi ya kidemokrasia.

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog