Wednesday, February 12, 2014


Serikali ya Afrika Kusini inachunguza uwezekano wa kuwasilisha ombi la kuandaa mashindano ya Jumuiya ya Madola au Commonwealth mwaka wa 2022. Rais wa kamati ya olimpiki nchini Afrika, Kusini Gideon Sam, amesema ana nia ya kuomba mashindano hayo kuandaliwa barani Afrika kwa mara ya kwanza. ''Naamini huu ni wakati wa Afrika kuandaa mashindano hayo'' Alisema Bwana Sam. Msemaji wa baraza la michezo nchini Afrika Kusini, amethibitisha kuwa waziri wa michezo, Fikile Mbalula, tayari amepokea ombi hilo na kuwa analiunga mkono. Akiongea na BBC, Sam, amesema kuwa Afrika Kusini, ina uwezo wa kuanda mashindano hayo ya Madola kwa kuwa taifa lake lina miundo mbinu ya kutosha na pia ujuzi wa kuandaa mashindano mengine ya kimataifa.

Wizara ya michezo nchini Afrika Kusini, sasa inatarajiwa kushirikiana na kamati ya olimpiki nchini humo, kabla ya kuwasilisha ombi hilo rasmi kwa baraza la mawaziri, ambalo litakuwa na uamuzi wa mwisho, ikiwa taifa hilo linaweza kuwa mwenyeji wa mashindano hayo. Afisa huyo amesema mji utakaoandaa mashindano hayo utaamuliwa baada ya maafisa wa mabaraza ya miji ya Durban, Cape Town na Johannesburg kuwasilisha rasmi maombi yao. Bwan Sam vile vile ni naibu rais wa Kamati kuu ya mashindano ya Jumuiya ya Madola, Commonwealth Games Federation (CGF), kamati ambayo inajukumu la kuandaa mashindano hayo. Mwezi uliopita, CGF, ilielezea wasi wasi wake kuwa hakuna taifa ambalo lilikuwa limeonyesha nia yake ya kuandaa mashindano hayo mwaka wa 2022, huku muda wa mwisho kwa kutuma maombi ni mwezi ujao. Hata hivyo nchi zinazodhamiria kuwa mwenye wa mashindano hayo zimepewa hadi mwaka wa 2015 kutuma maombi yao.

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog