Friday, September 18, 2015



Na Saleh Ally
LIGI Kuu Tanzania Bara msimu huu inaweza kuwa ndiyo pekee au ya kwanza ambayo ina viwanja vingi vilivyofanyiwa ukarabati.


Siku za nyuma ligi hii huenda ndiyo ilikuwa ligi kubwa zaidi Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati iliyopigwa kwenye viwanja vyenye viwango vya chini kabisa.

Uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya, Nangwanda Sijaona (Mtwara), Ali Hassan Mwinyi (Tabora) na Samora (Iringa), vilikuwa kati ya viwanja vyenye malalamiko makubwa kutokana na ubovu.

Ilionekana wazi kwa asilimia 90, viwanja vya Jiji la Dar es Salaam pekee ndiyo vilikuwa na ubora unaowezesha angalau wachezaji ‘kuinjoy’ soka kutokana na ubora unaotakiwa.

Angalau CCM Kirumba ule wa Mwanza, uliendelezwa ubora wake katika eneo la kuchezea. Hivyo kufanya ligi ionekane ni ya Dar peke yake.


Si Chama cha Soka Tanzania (Fat) wakati huo au klabu ambazo ziliamini suala la kurekebisha uwanja katika sehemu ya kuchezea ni jambo muhimu kwa ajili ya maendeleo ya soka nchini.

Asilimia kubwa ya viongozi wa Fat, hata baada ya kubadilika kuwa TFF walionekana kujali zaidi suala la mapato. Waliangalia wanaingiza kiasi gani cha fedha.

Upande wa klabu hali kadhalika, nao walionekana pia kujali mapato katika mechi wanazocheza kwenye viwanja vyao na si sehemu ya kuchezea uwanja zinakuwaje.

Hata wamiliki wa viwanja, mfano serikali au CCM ambao wanamiliki viwanja kadhaa, bado walionekana zaidi wakijali mapato na si wachezaji wanawezaje kucheza katika hali hiyo.


Hawakujali afya za wachezaji hao kutokana na kucheza kwenye viwanja vyao hivyo vya kiwango cha chini kabisa! Bado hawakuona kama ni sawa kuwa na viwanja bora vingesaidia kupanda haraka kwa ubora wa viwango katika Ligi Kuu Bara.

Viongozi wa klabu, TFF na wamiliki wa viwanja walikuwa tayari kutumia fedha zao hata kwa gharama kubwa kwa ajili ya kuimarisha mageti ili wadhibiti mapato lakini si viwanja.

Kelele za wanahabari, naamini zilichangia kupatikana kupatikana kwa mabadiliko kiasi fulani.

Mfano mabadiliko ya Uwanja wa Sokoine ambao miaka nenda rudi, ulikuwa tatizo kubwa na ligi ilichezwa ukiwa una kokoto ndani yake, jambo ambalo lilikuwa aibu kubwa kwa ligi kubwa zaidi Tanzania kuchezwa hapo.


Madaktari wa timu nyingi walilalamika kuhusiana na uwanja huo na vingine lakini safari hii, Azam TV inaonekana kuyakimbiza mabadiliko harakaharaka.

Azam TV imekuwa ikionyesha mechi za Ligi Kuu Bara moja kwa moja au Live kama ilivyo maarufu. Hali hiyo imechangia kuonyesha ubovu wa viwanja vingi tofauti na ilivyokuwa awali.

Kwa kuwa ni magazeti ndiyo yalipiga kelele sana kwa kushirikiana na redio. Viongozi wa klabu, mashirikisho na wamiliki wa viwanja waliweza kufanya propaganda kwamba havikuwa vibaya sana.

Utaona leo Uwanja wa Kaitaba wa mjini Bukoba umetafutiwa udhamini na hivi karibuni uwekaji wa nyasi bandia utakamilika.


Kaitaba ulikuwa ukionekana kituko katika Ligi Kuu Bara msimu uliopita. Marekebisho ya Uwanja wa Kambarage, Shinyanga wakijua wataonekana live kwenye Azam TV.
Msimu uliopita, Mkwakwani mjini Tanga ulikuwa tatizo. Mara baada ya msimu kwisha wakafanya marekebisho kuhakikisha sehemu ya kuchezea iko bora, hilo limefanyika.

Kwa maana hiyo hakuna ubishi kwamba Azam TV imekuwa ni sehemu ya mabadiliko ya haraka ya viwanja ambayo ni maendeleo ya soka.

Angalau viongozi wa klabu leo wanaweza kuwahoji wamiliki wa viwanja kufanya mabadiliko kutokana na muonekano unaokatisha tamaa Azam TV inapoonyesha mechi live. Lakini hata TFF na Bodi ya Ligi

Tanzania (TPLB) nao wanaona haya sasa. Kwamba ligi wanaoiongoza inaonekana kuchezwa katika sehemu duni kabisa huku wao wakikunja mamilioni ya wadhamini ambao pia watakuwa wanahitaji ubora wa muonekano ili kuthibitisha kwamba wanafanya kazi na watu makini wanataka maendeleo ya dhati.

Huenda siku zinavyokwenda, mechi za moja kwa moja kwenye Azam TV, zinaweza kusaidia kuwaamsha wadau wengi na kuusaidia mpira wa Tanzania uzidi kupanda zaidi kimaendeleo.

Wadau wakitaka maendeleo yapatikane zaidi, yale ambayo yanaonekana ni tatizo kupitia runinga hiyo ambayo sasa inazisumbua runinga kubwa kama SuperSport wanalazimika kukubali na kurekebisha kila wanayoona yamevumbuliwa na Azam TV na yanaonekana kuwa kikwazo cha maendeleo ya haraka ya soka

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog