Wednesday, October 22, 2014

MSANII wa Muziki wa Kizazi kipya nchini,Naseeb Abdul maarufu kama Diamond Platnumz anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa mahojiano baada ya kuonekana na mavazi halisi ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania katika Tamasha la Fiesta lililofanyika jijini Dar mwishoni mwa wiki.
Diamond amejikuta akifikia hatua hiyo ikiwa ni siku moja tu baada ya Meneja wake Babu Tale kamatwa na jana kwa kuhojiwa na kulala mahabusu kuhusiana na matumizi hayo ya mavazi ya kijeshi katika onyesho la Fiesta mwishoni wiki.
Kufuatia tukio la Diamond Platinumz kuonekana akiperform na sare zinazoaminika kuwa za jeshi la Wananchi (JWTZ), imeelezwa kuwa jeshi la Polisi limemshikilia meneja wa Diamond, Babu Tale na inaelezwa kuwa alilala selo.

Kwa mujibu wa chanzo chetu kilichokuwa katika eneo la kituo cha polisi cha Osterbay, Dar es Salaam jana (October 21), Babu Tale alifikishwa katika kituo hicho ambapo maafisa kadhaa wa jeshi na polisi walionekana katika eneo hilo.

Chanzo hicho kimeeleza kuwa Uongozi wa Diamond ulipewa muda wa kujieleza kabla ya saa mbili asubuhi, October 21 lakini haukufanya hivyo na ndipo hatua hiyo ikachukuliwa. Haijafahamika bado kwa nini jeshi la Polisi lilimshikilia Babu Tale peke yake bila Diamond lakini vyanzo vimeeleza kuwa mwanamuziki huyo yuko safarini. Hadi habari hii inaenda hewani, namba ya simu ya Babu Tale ilikuwa haipatikani.

Tovuti ya Times Fm imeongea na kamanda wa polisi wa mkoa wa kipolisi wa Kinondoni, Dar es Salaam, Camillus Wambura ambaye amesema bado hajawasiliana na kituo cha Osterbay kuhusu suala hilo na hajapata taarifa kwa kuwa kesi hiyo inachunguzwa na iko chini ya mkuu wa upelelezi wa Mkoa.

“Mimi ninachojua kuwa suala hilo liko chini ya uchunguzi. Habari ya kushikiliwa watu na mimi bado sijafahamu. Najua tu suala hilo liko chini ya uchunguzi na linafanyiwa uchunguzi. Hiyo ni kesi ambayo iko chini ya mkuu wa upelelezi wa Wilaya, chini ya mkuu wa upelelezi wa Mkoa. Kwa hiyo sijapokea taarifa ya uchunguzi huo ulipofika.” Ameiambia tovuti ya Times Fm.


Akijibu kuhusu taarifa za uongozi wa Diamond na Diamond kupewa muda wa kujieleza, Kamanda Wambura alijibu:
“Uchunguzi unafanywa huko. Kwa sasa hivi sina taarifa hiyo nina mambo mengi sana. Kwa hiyo kwa sasa hivi uchunguzi unafanywa chini ya Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa. Kwa hiyo sijapata nafasi ya kujua wamefikia wapi katika uchunguzi wa suala hilo,”ameongeza kamanda Wambura.

Mapema wiki hii, jeshi la wananchi Tanzania lilitoa taarifa kwa vyombo vya habari likipiga marufuku raia kuvaa sare za jeshi.

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog