Thursday, February 6, 2014


Bunge la Tanzania
Serikali ya Tanzania imekanusha taarifa za vyombo vya habari zilizodai kuwa wabunge wa nchi hiyo watalipwa kiasi cha zaidi ya dola laki moja za kimarekani watakapomaliza muda wao wa kipindi cha miaka mitano yakiwa malipo ya kiinua mgongo.
Taarifa ya wizara ya fedha imesema habari hiyo ni ya upotoshaji kwa kuwa Waziri wa fedha ,hakuwahi kuzungumza na mwandishi yeyote kama inavyodaiwa kuwa alithibitisha taarifa hizo.
Baada ya kuzuka kwa taarifa hizo baadhi ya wabunge waliozungumza na vyombo vya habari walikiri kuwepo kwa mipango hiyo huku wengine wakikanusha kuwa hawajawahi kupitisha mapendekezo kama hayo bungeni.
Naye naibu spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai ameiambia BBC kuwa habari hizi si za kweli '' nipende kusema kuwa jambo hilo kwa kweli si la kweli.Si la kweli kwa sehemu mbili,kwanza kwa utaratibu wa utawala wetu bora Tanzania, hakuna mtu mwenye mamlaka ya kujiongezea yeye mwenyewe kipato chake katika utumishi wa uma.kila ambaye ana mshahara au marupurupu ya aina fulani lazima yaidhinishwe na mamlaka au chombo kingine, ndio utaratibu wa utawala wetu.Kwa hiyo na sisi Bunge hatuna mamlaka ya kujipangia posho ya aina yoyoyte au mshahara wa aina yoyote kwa wabunge au viongozi wa Bunge''.
Pia naibu spika Ndugai amesema madai ya baadhi ya Wabunge kuwa kulikuwa na mpango huo si ya kweli na hayajawahi kujadiliwa katika Bunge hilo.
Taarifa hizo zilisababisha malalamiko kutoka kwa wananchi kuhusu hatua ya serikali kuwapatia wabunge kiasi hicho kikubwa cha fedha huku ikidai kuwa haina fedha za kutekeleza miradi kwa ajili ya huduma nyingine za umma.

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog