Saturday, October 19, 2013

Kukamatwa kwa washukiwa 11 wa al-Shabaab waliokuwa wakifanya mafunzo ya kijeshi katika mkoa wa Mtwara mapema mwezi huu kumeibua wasiwasi miongoni mwa wachambuzi wa usalama na maofisa kwamba kikundi hicho cha wanamgambo kinajaribu kudanganya walalamikaji wa Tanzania katika jitihada za kupanua eneo lake la ushawishi.
  • Picha ya skirini ya video ya lugha ya Kiswahili iliyotolewa na Al-Kataib, kitengo cha habari cha Shabaab.  Katika video hiyo, mwanamgambo ambaye anajulikana kwa jina la Abu Tarub al-Kenyi alieleza kwa watazamaji namna ya kutumia AK-47. [File] Picha ya skirini ya video ya lugha ya Kiswahili iliyotolewa na Al-Kataib, kitengo cha habari cha Shabaab. Katika video hiyo, mwanamgambo ambaye anajulikana kwa jina la Abu Tarub al-Kenyi alieleza kwa watazamaji namna ya kutumia AK-47. [File]
Washukiwa hao walikamatwa katika mlima wa Makolionga katika wilaya ya Nanyumbu tarehe 7 Oktoba na walikutwa wanamiliki silaha za moto, mapanga na DVD 25 zenye miongozo ya mafunzo ya al-Shabaab, kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mtwara Zelothe Stephen.
"Moja ya DVD waliyokutwa nayo ilikuwa na programu yenye jina Zinduka Zanzibar," aliiambia Sabahi, maana yake "Amka Zanzibar". "Ilifundisha namna ya kuua kwa haraka na kutoa mafunzo kwa wanamgambo. DVD nyingine zilikuwa na mafunzo yanayohusu ugaidi yanayohusiana na al-Shabaab."
Mamlaka za ndani zinachambua ushahidi huo na kuwatafuta washukiwa wengine katika eneo hilo pamoja na msaada wa vyombo vya upelelezi kutoka makao makuu ya polisi huko Dar es Salaam, Stephen alisema.
Jina lake ni Mohammed Makande mwenye umri wa miaka 39 kama kiongozi kinara wa washukiwa waliokamatwa. Washukiwa wengine walibainishwa kama: Said Mawazo (miaka 20), Ismail Chande (miaka 18), Abdallah Hamisi (miaka 32), Ramadhani Rajabu (miaka 26), Salum Wadi (miaka 38), Hassan Omary (miaka 39), Fadhili Rajabu (miaka 20), Abbas Muhidini (miaka 32), Issa Abeid (miaka 21) na Rashid Ismail (miaka 27).

Kuenea kwa wasiwasi

Wachambuzi wa usalama wasema serikali lazima iboreshe jitihada za kushuhulikia malalamiko ya ndani kuondoa msimamo mkali na kuanza kwa vurugu katika maeneo ambayo tayari yameshakosa utulivu.
Gideon Shoo, mwandishi wa habari mkongwe na mmiliki wa G&S Media Consultants, alisema al-Shabaab walikuwa hasa wakilenga Mtwara na Zanzibar ili kutumia hali iliyopo ya malalamiko ambayo wakaazi wanaweza kuwa nayo dhidi ya serikali.
"Kila mmoja anajua udhaifu huko Mtwara kuhusiana na uchimbaji wa gesi, na kuangalia kile kinachotokea huko Zanzibar pamoja na mashambulio ya asidi," Shoo aliiambia Sabahi. "Siyo siri kwamba al-Shabaab wanapanga kutumia hali ya kutoridhika katika maeneo hayo kama njia ya kuingilia Tanzania."
Shoo alisema serikali ya Tanzania inapaswa kuzungumza na Wazanzibari kufikia suluhisho ya kirafiki na la hakika kutatua malalamiko yanayohusiana na sehemu yao katika serikali ya umoja.
Kinyume chake, alisema, serikali lazima ihusishe wakaazi wa Mtwara na kutoa taarifa zaidi kuhusu faida muhimu zitakazotokana na kusafirisha gesi kutoka Mtwara kwenda Dar es Salaam, ambayo ilikuwa sababu kuu ya vurugu na ukosefu wa utulivu katika mkoa mapema mwaka huu.
Oswald Kasaizi, mkurugenzi mtendaji wa Msaada kwa Chama cha Maendeleo, asasi isiyo ya kiserikali ambayo inatoa msaada kwa jamii katika maeneo yenye mizozo, alisema habari za mafunzo ya washukiwa wa al-Shabaab nchini Tanzania ni mwanzo wa wasiwasi.
"Ukweli kwamba watu hawa wamefanikiwa kukutana pamoja na kuanza mafunzo katika ardhi yetu ni ishara mbaya sana," alisema.
Kasaizi alisema majeshi ya usalama yanapaswa kuwa makini na taarifa kuhusu vitabu vya mafunzo ya al-Shabaab yaliyokusudiwa kuishawishi Wazanzibari kwa sababu kikundi cha wanamgambo kinatumia maeneo ambayo tayari yana mgogoro kama eneo zuri kwa ajili ya operesheni zao.
"Al-Shabaab na al-Qaeda sasa wanatumia Zanzibar kama njia ya kuingilia," aliiambia Sabahi. "Lengo lao ni nchi nzima ya Tanzania na Bara la Afrika kwa ujumla. Hili ni tishio kubwa lililowahi kutokea. Mafunzo nchini kwetu yanahakikisha kwamba wapo hapa."
Kasaizi alilaumu mfumo wa usalama nchini kwa kuruhusu hali ya al-Shabaab kuanzisha kambi ya mafunzo katika ardhi ya Tanzania kwa mara ya kwanza.
"Jeshi letu la usalama limeonyesha kiwango kisichokubalika cha uzembe ambacho kinaweza kuigharimu nchi yetu kwa kiasi kikubwa," alisema.

Sio tukio pekee

Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya jinai Robert Manumba alisema mamlaka hazichukulii kirahisi tatizo la vitisho vya ugaidi na linajitahidi kusambaratisha makundi ya magaidi na mitandao yao.
"Tuna maelekezo kuhusu kuwepo kwa al-Shabaab na tunawafuatilia kwa karibu," aliiambia Sabahi.
"Kilichotokea huko Mtwara sio tukio pekee," alisema. "Inatokea hivyohivyo nchini Kenya, Uganda, Sudan, Somalia, Ethiopia na nchi nyingine nyingi, lakini kila inapotokea tunapeana taarifa katika njia ya kufuatilia mwenendo na kutafuta suluhisho."
"Mara kwa mara tunabadilishana taarifa za usalama kikanda na kimataifa," alisema Manumba.
Hii ni nyongeza ya Operesheni Kimbunga ya Serikali, ambayo inakusudia kuwarejesha kwao wahamiaji haramu nchini Tanzania.
"Kati ya tarehe 10 Septemba na Oktoba 10 tulifanikiwa kuwarejesha kwao zaidi ya wahamiaji haramu 22,000," alisema, akiongeza kwamba kutokana na upelelezi wa polisi, wahamiaji wengi walikuwa wakijihusisha na shughuli haramu.
Manumba aliwashukuru wananchi wa Mtwara kwa kuwatonya mapolisi kuhusu washukiwa wa ugaidi na kuwaagiza Watanzania kuendelea kuripoti kwa mamlaka zinazohusika kuhusu jambo lolote linalotiliwa wasiwasi ili kuhakikisha usalama.

Kurejesha mfumo wa nyumba kumi

Mjumbe wa Baraza la Kata ya Kitunda Israel Kimune aliiomba serikali kurejesha mfumo wa nyumba kumikumi ambao ulikuwa na mamlaka kitaifa wakati wa utawala wa Rais Julius Nyerere.
Chini ya mfumo huo, kila nyumba kumi zilizo karibu zilibainishwa kuwa chini ya kiongozi aliyewajibika kubainisha na kumwandikisha kila mmoja katika eneo lake, hata wageni na muda wao wa kuishi katika eneo hilo.
"Ninaelewa wazo la [mfumo] nyumba kumi lilitokana na [chama tawala] Chama Cha Mapinduzi, kisha wapinzani hawakujisikia vizuri kuufuata na ulifutwa kisheria, lakini tulifanya kosa kubwa," Kimune aliiambia Sabahi. "Unapaswa kurejeshwa kwa ajili ya usalama."
Naibu waziri wa Mambo ya Ndani Pereira Ame Silima alisema serikali ilikuwa ikizingatia kurejesha mfumo huo.
"Ulifanya kazi vizuri wakati wa mfumo wa chama kimoja lakini ulifutwa baada ya kuja kwa siasa za vyama vingi," Alisema Silima tarehe 11 Oktoba katika mahojiano na gazeti la serikali la Daily News.
Silima alisema maofisa polisi 8,000 wamekuwa wakisambazwa nchi nzima kuhakikisha kwamba ulinzi wa jamii unaimarishwa. "Mipango pia inafanyika kuangalia kwamba kila tarafa inakuwa na inspekta wa polisi anayeisimamia, sio kama sasa ambapo inspekta anawajibika kwa ngazi ya wilaya," alisema.

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog