Monday, July 27, 2015

 

LowassaNi wiki ya mtikisiko. Hivi ndiyo unavyoweza kuelezea hali itakavyokuwa nchini kutokana na matukio makubwa ya kisiasa yanayotazamiwa kutokea ndani ya wiki inayoanza leo ambayo yanaweza kubadili mwelekeo wa siasa za Tanzania.
Hali hiyo inatokana na vuguvugu la kisiasa linalohusisha viongozi wenye ushawishi kuhama vyama vyao vya siasa na kutimkia kwenye vyama vingine, ikiwa ni siku chache kabla ya kufanyika Uchaguzi Mkuu Oktoba 25, mwaka huu.
Ni wiki ambayo itapambwa na matokeo ya kikao cha Baraza Kuu la Uongozi wa CUF kilichofanyika jana mjini Zanzibar kuhusu mustakabali wake ndani ya Ukawa, ikizingatiwa kuwa hivi karibuni chama hicho kiliamua kujiweka kando ya vikao vya umoja huo hadi vikao vya juu viamue. 
Hata hivyo, habari ambazo gazeti hili limezipata zinasema kuwa uwezekano wa chama hicho kujitoa ndani ya Ukawa ulikuwa mdogo kutokana na kuogopa hasira za wananchi wenye matumaini na umoja huo.
Aidha, kulikuwa na taarifa kuwa kikao cha jana kilikuwa kinaangalia jinsi watakavyoshiriki katika umoja huo na kwamba kulikuwa na matumaini makubwa.
Vile vile, hii ni wiki ambayo kura za maoni zinazoendelea katika vyama vikubwa vya siasa, kuonyesha baadhi ya vigogo wakiangushwa na kujaribu kutafuta upenyo wa madaraka katika vyama vingine.
Pia, ni wiki ambayo chama kikuu cha upinzani, Chadema kimeamua kusogeza mbele tarehe za kuchukua na kurejesha fomu za kuomba kuteuliwa kugombea urais kutoka jana hadi Ijumaa, katika kile kinachotazamwa kama kusubiri mchakato wa kumpata mgombea urais.
Kana kwamba hiyo haitoshi, hii ni wiki ambayo minong’ono ya waziri mkuu wa zamani Edward Lowassa ambaye jina lake limekatwa katika orodha ya wasaka urais wa CCM anaweza kuhamia Chadema.
Tayari baadhi ya viashiria vya hali hiyo vimeanza kuonekana ambapo wiki iliyopita wabunge wawili wa chama tawala cha CCM, James Lembeli na Ester Bulaya waliachana na chama hicho na kujiunga na Chadema huku chama hicho cha upinzani kikitamba kujiandaa kuwapokea vigogo wengine zaidi.

Kiashiria kingine cha mtikisiko ni hatua ya madiwani 18 wa CCM wilayani Monduli na wengine 10 wa UDP na CCM Bariadi kuhamia Chadema.
Lakini pia wapo wabunge na madiwani wanaohama Chadema kwenda chama cha ACT-Wazalendo.

Vuguvugu hilo la kisiasa limekolezwa na kauli za wanasiasa wawili vijana kwa nyakati tofauti, Godbless Lema na Zitto Kabwe kuwa wiki hii itakuwa ya mshikemshike kutokana na mambo yaliyopangwa kufanyika.

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog