Monday, November 23, 2015


RAIS wa Real Madrid Florentino Perez ameitisha Mkutano na Wanahabari utakaofanyika Leo Saa 3 na Nusu Usiku kwa Saa za Bongo na hili limekuja mara baada ya Jumamosi kutandikwa 4-0 na Barcelona kwenye El Clasico iliyochezwa Nyumbani kwao Santiago Bernabeu.
Wakati Real inacharangwa na Barca Juzi Jumamosi, Mashabiki wa Real waliokuwepo Uwanjani Bernabeu walimtaka Perez ajiuzulu lakini hili Leo halitegemewi na hata kutimuliwa Kocha Rafa Benitez nako hakutarajiwa.
Wadau wengi wa Real wanamlaumu Perez kwa kuingilia upangaji Timu na kung’ang’ania kuchezeshwa Wachezaji wakubwa hata kama wamedorora na kuachwa Wachezaji ambao wako kwenye fomu.
Mwaka 2006, Mashabiki walimgeukia na kumsakama Perez ambae ghafla alibwaga manyanga na kuachia wadhifa wake wa Urais.
Mkutano huo wa Leo na Wanahabari umekuja baada ya mapema Leo Bodi ya Real kuketi kutafakari kipigo chao kutoka kwa Barca. 
Ushindi wa Barca wa Jumamosi umewafanya wawe Pointi 6 kileleni mbele ya Real ambapo wameporomoka hadi Nafasi ya 3 baada ya Atletico Madrid Jana kuifunga Real Betis 1-0 na kushika Nafasi ya Pili.
Benitez, aliewahi kuzifundisha Valencia, Liverpool, Inter Milan, Chelsea na Napoli, ni Meneja wa 10 chini ya himaya ya Perez na alitwaa wadhifa huo mwishoni mwa Msimu uliopita kutoka kwa Carlo Ancelotti. Ikiwa Benitez atatimuliwa, Wadau wengi wanahisi Gwiji la France Zinedine Zidane, ambae sasa anaifundisha Timu B ya Real, ndie atakaepewa Timu.Mechi inayofuata kwa Real ni hapo Jumatano Ugenini huko Ukraine wakicheza na Shakhtar Donetsk katika Mechi ya Kundi A la UEFA CHAMPIONS LIGI ambao wao washafuzu kuingia Raundi ya Mtoano ya Timu 16 huku wakiwa na Mechi 2 mkononi.
Ikiwa Real wataifunga Shakhtar basi watajihakikishia kufuzu toka Kundi A wakiwa ndio Vinara.

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog