Friday, July 17, 2015



Kocha wa Mkuu wa Yanga, Hans Van Pluijm (kulia) akisisitiza jambo kwa kuinua kidole juu na kufanya ukumbi kuzizima kwa kicheko alipokuwa akiongea na wandishi wa habari juu ya mchezo wao dhidi ya Gor-Mahia utakaochezwa kesho kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam. Katikati ni kocha mkuu wa Gor Mahia, Frank Nuttal na kushoto ni Katibu Mkuu wa Vyama vya Soka vya nchi za Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) Nicholaus Musonye. (Picha na Rahel Pallangyo)

MAKOCHA wa timu za Yanga na Gor Mahia ya Kenya wametambiana kila mmoja kuibuka na ushindi kwenye mchezo wa ufunguzi wa Mashindano ya kombe la Kagame utakaochezwa kesho majira ya saa 10:00 kwa saa za Afrika Mashariki kwenye Uwanja wa Taifa.
Kocha wa mkuu wa Yanga Hans Van Pluijm amesema anawaheshimu wapinzani wake timu ya Gor Mahia lakini haiogopi na ana matumaini makubwa ya kuibuka na ushindi kwenye mchezo huo.
“Nimefundisha soka Afrika tangu mwaka 1996 hivyo nina uzoefu na soka la timu za hapa kwa muda mrefu, lakini pia tumefanya maandalizi ya kutosha lakini mimi sidharau mpinzani wangu kwa sababu kwenye soka lolote linaweza kutokea na hakuna mtu anayejua matokeo”, amesema Pluijm.
Kocha mkuu wa Gor Mahia, Frank Nuttal amesema hana uzoefu mkubwa kwenye soka la Afrika ukilinganisha na mpinzani wake (Van Pluijm) lakini akasisitiza kuwa vijana wake wako vizuri kuikabili Yanga.
“Yanga ni timu kubwa japo sijawahi kuiona ikicheza lakini naamini ni timu yenye ushindani na mechi ya kesho itakuwa ngumu lakini mwisho wa mchezo tutajua matokeo”, amesema Nuttal.
Mchezo huu ambao mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri wa Ujenzi, John Magufuli ambaye pia ni mteule wa kugombea kiti cha urais kupitia chama tawala (CCM) unatarajiwa kuwa na msisimko wa aina yake kutokana na timu zote kuwa na historia inayolingana kwenye mashindano haya kwani kila mmoja ametwaa kombe la Kagame mara tano.

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog