Thursday, September 11, 2014


Na Baraka Mpenja, Dar es salaam
KOCHA mkuu wa Mbeya City fc na kocha bora wa ligi kuu Tanzania bara msimu uliopita, Juma Mwambusi, amewakaribisha makocha Patrick Phiri wa Simba na Marcio Maximo wa Yanga.
Akizungumza mchana huu na MPENJA BLOG, Mwambusi amesema kocha Phiri ana historia ya kufundisha soka la Tanzania kwa ngazi ya klabu wakati Maximo amefundisha timu ya Taifa, lakini wote wataleta changamoto nzuri kwake.
Mwambusi aliongeza kuwa ujio wa makocha wapya unaleta vionjo vipya katika ligi, lakini yeye kama mwalimu anajipanga kukabiliana kwa nguvu zote ili kuendeleza mafanikio ya msimu uliopita.
“Mimi naona tungoje dakika 90 zitakuwa zinatoa majibu. Sina la kusema zaidi ya kusema ni changamoto. Mwalimu mpya anapopatikana katika ligi anakuja na kionjo kipya, kama mwalimu lazima ukabiliane nacho. Kwahiyo sisi tunawakaribisha ligi kuu Phiri na Maximo.” Alisema Mwambusi.
Aidha, Mwambusi alifafanua kuwa maandalizi ya ligi kuu yanakwenda vizuri  na wapo hatua za mwisho kabisa kuhakikisha wanapata kikosi cha kwanza.
Alisema mwishoni mwa wiki hii wanatarajia kupata mechi ya mwisho ya kirafiki itakayofunga mahesabu ya kuanza msimu mpya unaotarajia kuanza septemba 20 mwaka huu.
“Vijana wanaendelea vizuri na tuko katika kumalizia-malizia maandalizi na tunaangalia utaratibu wa kupata timu ya kucheza mechi ya kirafiki ili kupata kikosi cha kwanza”
“Wachezaji wote wako katika hali nzuri, kikubwa tunadhani mwishoni mwa wiki hii tutakuwa na mechi ya kirafiki ambayo itakamilisha maandalizi yetu na tujue tunatokaje katika mechi za ligi kuu.”
“Bado viongozi wanafanya jitihada  kupata timu kutoka Malawi na ikishindikana tutacheza na timu ya hapa ndani ambayo itatupa upinzani mzuri”
 Kocha huyo maarufu kwa sasa alisema soka sio mchezo wa kutabiri, lakini anashukuru kwa vile mwaka jana walitoa changamoto kubwa na timu nyingi zinataka kuwaiga wao.
“Mpira wa miguu sio wa kutabiri, lakini mimi nashukuru kwa kuwa mwaka jana Mbeya City fc tumeleta changamoto na watu wanajiandaa vizuri sana na kila mtu anataka kuona timu yake itafanyeje ili iweze kuwa kama Mbeya City. Mimi nafikiri ligi itakuwa na changamoto sana mwaka huu.
Msimu uliopita, Mbeya City ilishika nafasi ya tatu kwa pointi 49 nyuma ya Yanga walioshika nafasi ya pili na Azam fc nafasi ya kwanza (mabingwa).

Mbeya city wanatarajia kuanza kampeni zao za kusaka ubingwa msimu wa 2014/2015 septemba 20 mwaka huu  katika uwanja wa nyumbani wa Sokoine jijini Mbeya dhidi ya maafande wa JKT Ruvu.

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog