Monday, October 19, 2015



Na Saleh Ally
INAWEZEKANA kabisa ikawa ni vigumu sana kwa watu wengi kuona ni miujiza kwa kampuni kubwa wanayoijua kusikia imefeli na mwisho inafungwa kabisa. Yote yanawezekana ndiyo maana maduka makubwa ya bidhaa maarufu kama Uchumi Supermarket, yamefilisika.

Biashara inahitaji nidhamu ya juu sana, inahitaji kuwasoma wateja ambao sawa na wamiliki, wanataka nini, kwa wakati gani lakini pia kusikiliza shida au kero zao.

Mimi siamini kama Kampuni ya DSTV imekuwa ikisikiliza kero za wateja wake hasa kwa Tanzania, wengi wanalia na wako wameanza kuweka chuki kabisa.

Wote wanaolia ni kuhusiana na bei, kwamba zimekuwa kubwa sana hadi kufikia kuona kama ni sehemu ya kuwakomoa. Wako wanaoamini DSTV hawawajali wazalendo zaidi ya kuangalia kile wanachoingiza.

Maoni mengi huenda tumekuwa tukiyapata kwa kuwa wengi ambao wamekuwa wakiyatuma ni watu wa michezo, wanajua Championi ndiyo makao makuu ya michezo kama utazungumzia magazeti ya michezo, kweli hapa ndiyo nyumbani.
 
RAIS JAKAYA KIKWETE AKIWA NA MMILIKI WA AZAM MEDIA, SAID SALIM BAKHRESA PAMOJA NA BAADHI YA WAFANYAKAZI WA AZAM TV SIKU YA UZINDUZI WAKE, MIEZI MICHACHE ILIYOPITA. TAYARI AZAM TV IMEKUWA GUMZO KUTOKANA NA UBORA WA KAZI YAKE LAKINI BEI AMBAZO WAZALENDO WENGI WANAWEZA KUZIMUDU.
Wapenda soka wengi hasa barani Afrika ni watu masikini, lakini mpira au soka ni zaidi ya kabila na wengine ni zaidi hata ya dini, wanaupenda hadi kufikia kiwango cha kuonekana kama wendawazimu.

Ndiyo starehe kuu na tulizo la moyo, kama ukitokea kuwaingizia kero, hamtaelewana milele. Ndiko hili suala linapokwenda, kwamba itafikia DSTV na Watanzania wapenda soka au michezo wasiwe na urafiki hata kidogo.

Hii inatokana na kilio cha malipo ya mwezi, hasa kwa wale wanaotaka kuangalia Ligi Kuu England. Ili mtu apate nafasi ya kuangalia michezo ya moja kwa moja ya ligi hiyo, basi lazima alipe takribani dola 100 (wakati mwingine ni zaidi ya Sh 200,000). Kwa Mtanzania wa kawaida hakika ni fedha nyingi sana.

DSTV wanafanya biashara, hili hakuna anayeweza kukataa lakini bado kuna kila sababu ya kuangalia mbinu za kibiashara na kuwapunguzia Watanzania kwa kuwa wanapenda soka.

Nina rafiki zaidi ya watatu ambao wameamua kuhamishia mapenzi yao Hispania. Wanaamini La Liga ni bora kuliko Premier League lakini imekosa matangazo ya kutosha. Wanaona DSTV sasa inaitumia EPL kama silaha ya kuwakandamiza wanyonge na inawezekana kupunguzwa kwa bei.
KING'AMUZI CHA DSTV...
Wanajua kuwa Afrika Kusini kuna unafuu mkubwa wa bei ukilinganisha na hapa nyumbani Tanzania. Wanaendelea kuamini La Liga ambayo sasa wanaweza kuipata kwenye ving’amuzi vya Azam TV tena ikichambuliwa kwa lugha ya Kiswahili, itakata kiu yao.

Nina rafiki ambao sasa wanaangalia Premier League kupitia mitandao ambayo mtu anaweka ‘bando’ yake ya intaneti na kuangalia moja kwa moja mechi hizo.

Hawa ni wale wanaoondoka taratibu katika himaya ya DSTV ambao wanaona haiwezekani lakini nawasisitizia kadiri siku zinavyosonga wanaotafuta njia mbadala watakuwa wengi na watazidi kuachana nayo.

Azam TV ambayo pamoja na gharama za uendeshaji kuwa kubwa kama DSTV wanavyosema, lakini imejitahidi kuwapa Watanzania karibu kila kitu ambacho wanatoa DSTV na huenda zaidi, lakini gharama ziko chini.

Hii inafanya Watanzania wazidi kuongeza mapenzi na upande wanaoona unawajali. Najua kuna gharama kubwa kupata uonyeshaji wa EPL lakini bado kuna njia zinaweza kutumika kuwasaidia Watanzania katika suala la gharama za malipo ya mwezi.

Mara zote, mtu anamjali anayemjali. Hata kama kweli wanafanya biashara, DSTV wanatakiwa kuonyesha wanawajali Watanzania. Wajiulize, siku Azam TV wakipata nafasi ya kuonyesha moja kwa moja mechi za EPL, wao itakuwaje?

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog