Friday, July 4, 2014

MESSI-ARGENTINA2014DIEGO ARMANDO MARADONA, Lejendari wa Argentina, amesema Nchi yao inacheza chini ya kiwango, wanamtegemea sana Lionel Messi na lazima waongeze juhudi ikiwa watataka kuifunga Belgium kwenye Robo Fainali ya Kombe la Dunia ambayo watakutana Jumamosi Usiku.
Maradona amesema: “Bado hatujaanza! Lazima watambue wazi, waweke vichwani mwao, si kumtegemea Messi tu. Labda anaweza kufunga Bao safi…lakini kama hakuweza, wasimrukie Kijana huyu na kumfanya ndie mwenye hatia ya maafa ya Argentina!”
Maradona, ambae ndie alikuwa Kocha wa Argentina kwenye Fainali za Kombe la Dunia za Mwaka 2010 huko Afrika Kusini walikotolewa Robo fainali, alikuwa akihojiwa na TV ya Venezuela mara baada ya Argentina kuitoa kwa mbinde Switzerland kwa Bao 1-0 la mwishoni la Dakika za Nyongeza 30 lililofungwa na Angel Di Maria baada kazi njema ya Messi.
Akizungumzia Mechi hiyo, Maradona alisema: “Mtu kwa Mtu, na kwa pamoja, Argentina walikuwa bora, Wao [Uswisi] wanatengeneza Saa nzuri sana lakini wana Wanasoka wachache.”
Huko Brazil, Argentina wameshinda Mechi zao zote 4 hadi sasa na kufunga Bao 7 huku Messi akifunga Bao 4 kati ya hizo lakini ushindi wote huo ulikuwa wa tofauti ya Bao 1 tu.
Katika Mechi zote hizo 4, Messi ndie alieibuka na Tuzo ya Mchezaji Bora wa kila Mechi.
Maradona aliongeza “Huyu Kijana [Messi] yuko mpweke..Timu haibadilishi kasi yake, Mastraika hawazunguki. Nasikia uchungu, hasira, fedheha, kwa sababu Argentina inaweza kucheza vizuri zaidi, tena zaidi…Kocha lazima alazimishe hili! Kama hawataongeza ubora dhidi ya Belgium, basi tuko mashakani! ”
Argentina wameshatwaa Kombe la Dunia mara mbili na wakitwaa kwa mara ya 3, tena nyumbani kwa Mahasimu wao Wakuu Brazil, hiyo itakuwa starehe kubwa kwa Mashabiki wa Argentina ambao Maelfu yao wamefurika Brazil kushangilia Timu yao.

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog