Monday, December 23, 2013



Rais Dk. Jakaya Kikwete.
Stori: Mwandishi Wetu
MWAKA 2013 uko ukingoni. Matukio ni mengi yaliyoitikisa Tanzania, lakini hili la mawaziri wanne kung’oka limefunga mwaka vibaya, Ijumaa Wikienda lina cha kusema.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Khamisi Kagasheki.
Anga la siasa, uongozi na utawala limegubikwa na wingu zito ndani ya ‘kabineti’ kufuatia kujiuzuru kwa waziri mmoja na kung’oka watatu kwa kuwajibika kufuatia tuhuma za watendaji wao kutekeleza majukumu ndivyo sivyo.
Hali ya hewa ilianza kutibuka Ijumaa iliyopita bungeni mjini Dodoma wakati Kamati Ndogo ya Ardhi, Maliasili na Mazingira chini ya mwenyekiti wake,  James Lemberi kuwasilisha taarifa yake rasmi kuhusiana na yale yaliyojiri wakati wa Oparesheni Tokomeza Ujangili ikiwekwa bayana kwamba kulikuwa na ukiukwaji wa haki za raia wasiokuwa na hatia.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi.
Katika ripoti hiyo, Mheshimiwa  Lembeli (Mbunge wa Kahama Mjini, CCM) alianika matukio yaliyowakumba raia wakati wa utekelezaji wa oparesheni hiyo.
Alipokaa, waheshimiwa wabunge walianza kuchachamaa wakiwataka mawaziri hao kung’oka ili kuonesha kuchukizwa kwao na watendaji waliokuwa chini yao. Mawaziri hao ni Balozi Hamis Sued Kagasheki, Mathayo David Mathayo, Shamsi Vuai Nahodha na Emmanuel John Nchimbi.
Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamsi Vuai Nahodha.
KAGASHEKI ALICHEZWA NA MACHALE, AKAFUNGUA MLANGO
Mashambulizi makali yaliyojaa uchungu mkubwa, yalionekana kumgusa vilivyo aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Mh. Kagasheki, akatangaza kujiuzulu kwa hiyari yake hivyo kuibua hisia kuwa alichezwa na machale.
Tangazo la Kagasheki lilisindikizwa na kauli ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete ‘JK’ kupitia taarifa iliyowasilishwa bungeni na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akisema ametengua nafasi zingine tatu za mawaziri walioguswa na ‘mashambulizi’ ya wabunge. Rais yupo Marekani anacheki afya.
Mawaziri waliotajwa kwenye tamko hilo ni Waziri wa Mambo ya Ndani, Nchimbi (Mb), Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Nahodha na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Dk. Mathayo.
Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi , Dk David Mathayo.
WANAOKALIA KUTI KAVU
Aidha, kufuatia sekeseke hilo, vyanzo mbalimbali vya habari za ndani vimesema kuwa, mawaziri wanaotajwa kukalia kuti kavu katika nafasi zao ni pamoja na Waziri wa Maji, Prof. Jumanne Maghembe (Mb), Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Jumanne Kawambwa (Mb), Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mh. Hawa Abdulkadil Ghasia (Mb) na Waziri wa Fedha, Mipango na Uchumi, Dk. William Mgimwa (Mb).
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Jumanne Kawambwa (Mb).
Wengine ni Waziri wa Kilimo na Chakula, Eng. Christopher Chiza Kajoro (Mb) na Naibu wake, Mh. Adam Ali Kighoma Malima.
“Hao wanakalia kuti kavu katika panguapangua ya baraza la mawaziri itakayofanyika hivi karibuni kutokana na kiwango chao cha utendaji katika wizara hizo kuzorota, si unajua wamekuwa wakiitwa mizigo? Kwa hiyo kama kina Nchimbi wamelia bado vilio zaidi vinakuja,” kilisema chanzo chetu.
WANAOTAJWA KUINGIA
Habari zinadai kuwa katika fumuafumua inayotarajiwa kufanyika ndani ya baraza hilo, baadhi ya wabunge na manaibu waziri wanatajwa kuingia kwenye baraza hilo.
Dk. Asha-Rose Mitengeti Migiro (Mb kuteuliwa).
Wanaotajwa ni Dk. Asha-Rose Mitengeti Migiro (Mb kuteuliwa) kuwa waziri, Mh. Januari Makamba (naibu waziri wa sayansi, teknolojia na elimu ya juu) kuwa waziri kamili, Mh. Amos Makalla  (Mb) kuwa waziri kamili, Mh. Mwiguru Nchemba (Mb) kuwa waziri, Mh. Peter Serukamba (Mb) kuwa waziri, Mh. Faustine Ndungulile (Mb) kuwa waziri na Mh. Jenister Joachim Mhagama (Mb) kuwa waziri.
Naibu Waziri wa Sayansi, Teknolojia na Elimu ya Juu, Januari Makamba.
UTABIRI UMETIMIA
Kuondoka kwa mawaziri hao kunatimiza utabiri uliowahi kuanikwa mapema Aprili mwaka huu na mtabiri maarufu nchini, Maalim Hassan Yahya Hussein ambaye ni mrithi wa kazi za marehemu Yahya Hussein.
Mtabiri huyo aliwahi kutabiri kuwa, JK kwa mwaka huu atafanya maamuzi magumu ambayo yatashangaza wengi, hata kwa mataifa ya nje na hivyo kuandika historia.

0 maoni:

Post a Comment

waliotembelea blog